Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Alinisaidia Kukabiliana na Matatizo

Yehova Alinisaidia Kukabiliana na Matatizo

Simulizi la Maisha

Yehova Alinisaidia Kukabiliana na Matatizo

LIMESIMULIWA NA DALE IRWIN

“WANANE WANATOSHA! MAPACHA WANNE WAONGEZA KAZI.” Hicho ndicho kilichokuwa kichwa cha gazeti lililotangaza kwamba tumepata watoto wanne zaidi katika familia yetu yenye wasichana wanne. Nikiwa kijana, sikuwa na nia ya kuoa wala kuwa na watoto. Lakini sasa nilikuwa baba wa watoto wanane!

NILIZALIWA mwaka wa 1934 katika mji wa Mareeba, Australia. Mimi ndiye niliyekuwa mtoto wa mwisho katika familia yenye watoto watatu. Baadaye familia yetu ilihamia Brisbane, ambako mama yangu alikuwa mwalimu wa shule ya Jumapili ya kanisa la Methodisti.

Mapema katika mwaka wa 1938, magazeti yaliripoti kwamba huenda Joseph F. Rutherford kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova angekatazwa kuingia Australia. “Kwa nini wanamtendea hivyo?” Mama alimuuliza Shahidi aliyetutembelea nyumbani baada ya ripoti hiyo. Shahidi huyo alijibu: “Je, Yesu hakusema kwamba watu wangewatesa wafuasi wake?” Kisha Mama akakubali kijitabu kinachoitwa Cure, ambacho kilionyesha tofauti nyingi kati ya dini ya kweli na ya uwongo. * Kwa kuwa Mama alipendezwa na kijitabu hicho, alitupeleka sisi watoto kwenye mkutano wa Mashahidi wa Yehova Jumapili iliyofuata. Mwanzoni baba yangu alipinga vikali jambo hilo, lakini mara kwa mara aliandika maswali ya Biblia na kumwomba Mama ampe mmoja wa akina ndugu. Kisha ndugu aliyepewa maswali hayo aliandika majibu ya Kimaandiko na kumwomba Mama ampelekee Baba.

Jumapili moja baba yangu alihudhuria mkutano pamoja nasi akiwa na nia ya kueleza kwamba hakubaliani na Mashahidi. Hata hivyo, baada ya kuzungumza na mwangalizi anayesafiri ambaye alikuwa anatembelea kutaniko wakati huo, Baba alibadili mtazamo wake na hata akaruhusu nyumba yetu itumiwe kwa ajili ya funzo la Biblia la kila juma, lililohudhuriwa na watu waliopendezwa katika eneo letu.

Wazazi wangu walibatizwa Septemba 1938. Mimi, ndugu, na dada zangu tulibatizwa Desemba 1941 kwenye kusanyiko la kitaifa lililofanyiwa Hargreave Park huko Sydney, New South Wales. Nilikuwa na umri wa miaka saba. Baada ya hapo, nilishiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani pamoja na wazazi wangu. Siku hizo, Mashahidi walienda mlango kwa mlango wakiwa wamebeba kinanda cha gramafoni ili wenye nyumba wasikilize hotuba za Biblia zilizorekodiwa.

Shahidi mmoja ninayemkumbuka sana ni Bert Horton. Alikuwa na gari ambalo juu yake kulikuwa na kipaaza-sauti. Kufanya kazi na Bert kulifurahisha, hasa kwa mvulana wa umri wangu. Kwa mfano, mara nyingi tulipokuwa tukichezesha rekodi ya hotuba ya Biblia kutoka juu ya mlima, tungeona gari la polisi likija. Bert angesimamisha rekodi hiyo mara moja na kuendesha gari kwenye mlima mwingine, kisha kuchezesha rekodi nyingine. Nilijifunza mambo mengi kuhusu kumtegemea Yehova na ujasiri kutoka kwa Bert na ndugu wengine washikamanifu kama yeye.—Mathayo 10:16.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilitoa ushahidi kwa ukawaida baada ya shule nikiwa peke yangu. Wakati fulani, nilikutana na familia ya akina Adshead. Baada ya muda, wazazi wote wawili, watoto wao wanane, na wajukuu wao wengi walijifunza kweli. Namshukuru Yehova kwa kunitumia nikiwa mvulana mdogo kuisaidia familia hiyo nzuri kujifunza kweli ya Biblia.—Mathayo 21:16.

Kupata Mapendeleo ya Utumishi Nikiwa na Umri Mdogo

Nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilianza utumishi wa wakati wote nikiwa painia na kutumwa Maitland, New South Wales. Mwaka wa 1956, nilialikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Australia, huko Sydney. Kati ya wale 20 waliofanya kazi huko, theluthi moja hivi walikuwa watiwa-mafuta, wenye tumaini la kutawala pamoja na Kristo katika Ufalme wake mbinguni. Lilikuwa pendeleo kama nini kufanya kazi pamoja nao!—Luka 12:32; Ufunuo 1:6; 5:10.

Azimio langu la kuendelea kuwa mseja lilididimia nilipokutana na Judy Helberg, dada painia mwenye kuvutia ambaye alikuwa amealikwa kutumikia kwa muda kwenye ofisi ya tawi ili kunisaidia katika mradi fulani mkubwa. Mimi na Judy tulipendana, na baada ya miaka miwili tukafunga ndoa. Baadaye, tukaanza kazi ya mzunguko, ambayo ilitia ndani kutembelea kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova kila juma ili kuwatia moyo akina ndugu.

Katika mwaka wa 1960, Judy alimzaa binti yetu wa kwanza Kim. Siku hizi, mtu akipata mtoto analazimika kuacha kazi ya mzunguko na kukaa mahali pamoja. Lakini tulishangaa sana tulipoambiwa tuendelee kutembelea makutaniko. Baada ya kusali sana, tulikubali mwaliko huo, na katika miezi saba iliyofuata, Kim alisafiri pamoja nasi kilometa 13,000 kwa basi, ndege, na gari-moshi tulipotembelea makutaniko huko Queensland na Eneo la Kaskazini. Hatukuwa na gari wakati huo.

Nyakati zote tulikaa katika nyumba za akina ndugu na dada. Kwa sababu ya joto, siku hizo vyumba vya kulala vilikuwa na mapazia badala ya milango, na hilo lilitutatiza wakati Kim alipolia usiku. Hatimaye, ilikuwa vigumu sana kutekeleza wajibu wa kulea mtoto na kutimiza mgawo wetu. Kwa hiyo, tulikaa huko Brisbane, nami nikaanza kazi ya kuchora. Miaka miwili baada ya Kim kuzaliwa, tulipata binti mwingine, Petina.

Kukabiliana na Msiba

Katika mwaka wa 1972, wakati wasichana wetu walipokuwa na umri wa miaka 12 na miaka 10, Judy alikufa kutokana na ugonjwa wa Hodgkin. Familia yetu ililemewa sana na huzuni. Hata hivyo, Judy alipokuwa mgonjwa na baada ya kifo chake, Yehova alitufariji kupitia Neno lake, roho yake takatifu, na akina ndugu. Pia, tuliimarishwa na gazeti la Mnara wa Mlinzi ambalo tulipokea baada tu ya msiba huo. Lilikuwa na makala iliyozungumzia majaribu ya kibinafsi, kutia ndani kufiwa, nalo lilionyesha jinsi majaribu yanavyoweza kutusaidia kusitawisha sifa za kimungu kama vile uvumilivu, imani, na utimilifu. *Yakobo 1:2-4.

Baada ya kifo cha Judy, uhusiano wangu pamoja na binti zangu uliimarika zaidi. Lakini haikuwa rahisi kutimiza jukumu la baba na la mama. Hata hivyo, binti zangu wawili walikuwa wazuri nao walifanya mambo yawe rahisi zaidi.

Kuoa Tena na Kuwa na Familia Kubwa

Baada ya muda, nilioa tena. Mimi na mke wangu mpya, Mary, tulifanana kwa njia nyingi. Yeye pia alifiwa na mwenzi wake wa ndoa baada ya kuugua ugonjwa wa Hodgkin. Mary pia alikuwa na binti wawili, Colleen na Jennifer. Petina alimzidi Colleen kwa miaka mitatu hivi. Hivyo basi, familia yetu ikawa na wasichana wanne wenye umri wa miaka 14, 12, 9, na 7.

Mwanzoni, mimi na Mary tuliamua kwamba kila mtu angewatia nidhamu watoto wake mwenyewe mpaka wakati ambapo wale watoto wengine wangeweza kukubali kwa hiari kusahihishwa na mzazi wa kambo. Katika uhusiano wetu tukiwa mume na mke, mimi na Mary tulifuata sheria mbili muhimu. Kwanza, hatukubishana kamwe mbele ya watoto, na pili, kulingana na kanuni ya Biblia kwenye Waefeso 4:26, tulizungumza hadi tuliposuluhisha matatizo yetu, hata ikiwa mazungumzo hayo yangechukua saa nyingi!

Kila mtu alifanya mabadiliko ya kustaajabisha ili kuzoea maisha katika familia ya kambo, lakini tuliendelea kuwakumbuka wapendwa wetu waliokufa. Kwa mfano, Mary alilia kila Jumatatu usiku. Baada ya funzo letu la familia, wasichana walipoenda kulala, mara nyingi Mary alifunua hisia zake za moyoni.

Mary alitaka tupate mtoto. Inasikitisha kwamba mimba yake iliharibika. Mary alipokuwa mjamzito tena, jambo la kushangaza lilitukia. Baada ya kupimwa, ilionekana kwamba Mary angejifungua watoto wanne! Nilishtuka sana. Nilikuwa na umri wa miaka 47, na baada ya muda mfupi ningekuwa baba ya watoto wanane! Mapacha hao wanne walizaliwa kupitia upasuaji Februari 14, 1982, baada ya Mary kuwa mjamzito kwa majuma 32. Walifuatana hivi, Clint, kilo 1.6; Cindy, kilo 1.9; Jeremy, kilo 1.4; na Danette, kilo 1.7. Hawakufanana hata kidogo.

Baada tu ya watoto hao kuzaliwa, daktari wa Mary alikuja na kuketi kando yangu.

Aliniuliza: “Je, una wasiwasi kuhusu jinsi utakavyowalea watoto hao?”

Nikamwambia hivi: “Sijawahi kukabili hali kama hii.”

Maneno yake yaliyofuata yalinishangaza sana na kunitia moyo.

Alisema: “Kutaniko lenu halitawaacha. Mkiomba msaada, mtaupata haraka!”

Kwa sababu ya jitihada za daktari huyo na wahudumu wenzake wa afya, watoto wetu wanne wenye afya waliruhusiwa kutoka hospitalini baada ya miezi miwili tu.

Ugumu wa Kuwalea Mapacha Wanne

Ili kudumisha utaratibu, mimi na Mary tulipanga ratiba ya saa 24. Wasichana wanne wakubwa walisaidia sana kuwatunza watoto. Na maneno ya daktari yalitimia, kwa kuwa, hata tulipohitaji msaada mdogo, kutaniko lilikuwa tayari kutusaidia. Kabla ya wakati huo, rafiki yetu wa muda mrefu, John MacArthur alifanya mpango ili Mashahidi ambao ni mafundi wapanue nyumba yetu. Tulipowaleta watoto nyumbani kutoka hospitalini, akina dada kadhaa walitusaidia kuwalea. Fadhili zote hizo zilionyesha upendo wa Kikristo.—1 Yohana 3:18.

Kwa njia fulani, mapacha hao wanne walikuwa “watoto wa kutaniko.” Hata kufikia leo, watoto hao huwaona ndugu na dada wengi wenye upendo waliotusaidia kuwa sehemu ya familia yetu. Mary ni mke na mama wa pekee sana, naye amejitoa mhanga kuwatunza watoto wake. Ametumia kikamili mambo ambayo amejifunza katika Neno la Mungu na tengenezo Lake. Hivyo ndivyo vyanzo bora zaidi vya mashauri!—Zaburi 1:2, 3; Mathayo 24:45.

Kila juma, tulihudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki kazi ya kuhubiri kwa ukawaida, ingawa ilikuwa vigumu kufanya hivyo tukiwa na watoto wanne wachanga. Baraka moja ambayo tulipata wakati huo ni kujifunza Biblia pamoja na familia mbili ambazo zilikuja kwetu kwa ajili ya funzo. Ingawa hilo liliturahisishia mambo, nyakati nyingine Mary alichoka sana hivi kwamba alilala wakati wa funzo huku akimbeba mtoto mikononi. Hatimaye, watu hao wakawa ndugu na dada zetu wa kiroho.

Mazoezi ya Kiroho Wakiwa Wachanga

Hata kabla ya watoto hao kuanza kutembea, mimi, Mary, na wasichana wetu wakubwa, tulienda nao katika huduma ya shambani. Watoto hao walipokuwa wanajifunza kutembea, mimi nilienda na wawili na Mary akaenda pamoja na wale wengine wawili, nao hawakuwa mzigo. Mara nyingi, walituwezesha kuanzisha mazungumzo pamoja na wenye nyumba wenye urafiki. Siku moja nilikutana na mtu aliyedai kwamba ikiwa ulizaliwa siku inayolingana na ishara fulani ya nyota, utakuwa na tabia fulani. Sikubishana naye, bali nilimwomba nirudi baadaye asubuhi hiyohiyo. Alikubali, nami nikarudi na mapacha wote. Alitazama kwa mshangao huku nikiwapanga kulingana na jinsi walivyofuatana walipozaliwa. Kisha, tukawa na mazungumzo ya kirafiki, si tu kuhusiana na tofauti zao za kimwili bali pia kuhusu tofauti kubwa katika nyutu zao, na hilo lilikomesha ubishi wake. Alisema hivi: “Sijui kwa nini nilikueleza maoni hayo. Inaonekana ninahitaji kufanya utafiti zaidi.”

Wakiwa wachanga, wote wanne hawakupenda kutiwa nidhamu pamoja walipokosea, hivyo tulimsahihisha kila mmoja wao akiwa peke yake. Hata hivyo, walijifunza kwamba wote wanapaswa kufuata sheria zilezile. Walipokabili masuala ya dhamiri shuleni, walishikilia kwa uthabiti kanuni za Biblia na kutegemezana, huku Cindy akiwa msemaji wao. Punde si punde, watu walitambua kwamba huwezi kufanya mzaha na kikundi cha watu wanne!

Mimi na Mary tulikabili matatizo ya kawaida ya kuwasaidia watoto hao waendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova katika miaka yao ya utineja. Tunaweza kusema kwamba ingekuwa vigumu zaidi kufanya hivyo ikiwa hatungetegemezwa na kutaniko lenye upendo na chakula kingi cha kiroho ambacho tulipokea kutoka kwa sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova. Tulijitahidi kuwa na funzo la Biblia la familia kwa ukawaida na kudumisha mawasiliano, ingawa haikuwa rahisi nyakati zote. Lakini, jitihada zetu zimefanikiwa kwa sababu watoto wetu wote wanane wamechagua kumtumikia Yehova.

Kukabiliana na Uzee

Kwa miaka mingi nimefurahia mapendeleo mengi ya kiroho: kuwa mzee wa kutaniko, mwangalizi wa jiji, na mwangalizi wa mzunguko wa badala. Pia, nimetumikia nikiwa mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali, ambayo huwasaidia madaktari kushirikiana na wagonjwa Mashahidi wakati suala la kutiwa damu mishipani linapozuka. Kwa miaka 34 nimekuwa pia na pendeleo la kuandikisha ndoa kisheria. Nimesimamia sherehe 350 hivi za kuandikisha ndoa, kutia ndani zile za binti zangu sita.

Namshukuru Yehova daima kwa vile ambavyo niliungwa mkono kwa ushikamanifu kwanza na Judy, na sasa na Mary. (Methali 31:10, 30) Zaidi ya kuniunga mkono katika kazi ya kuwa mzee wa kutaniko, waliweka pia mfano mzuri katika huduma na kuwasaidia watoto wasitawishe sifa za kiroho.

Katika mwaka wa 1996, iligunduliwa kwamba nina ugonjwa fulani wa ubongo unaofanya mikono yangu itetemeke na kudhoofisha usawaziko wangu. Hivyo, singeweza kuendelea kuchora. Hata hivyo, bado ninapata shangwe nyingi sana ninapomtumikia Yehova, ingawa sina nguvu nyingi. Jambo zuri ni kwamba nimekuwa mwenye huruma zaidi kuwaelekea wengine waliozeeka.

Ninapofikiria maisha yangu, mimi humshukuru Yehova kwa kunisaidia mimi na familia yangu sikuzote kukabiliana na matatizo yetu mengi kwa shangwe. (Isaya 41:10) Mimi na Mary pamoja na watoto wetu wanane tunashukuru pia kwa kuwa na akina ndugu na dada wa kiroho ambao wanatuunga mkono. Wote wameonyesha upendo wao kwa njia nyingi sana.—Yohana 13:34, 35.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, lakini sasa hakichapishwi tena.

^ fu. 17 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1972, ukurasa wa 417-421 au gazeti la Kiingereza la Machi 15, 1972, ukurasa wa 174-180, au gazeti la Kifaransa la Julai 1, 1972, ukurasa wa 398-404.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nikiwa pamoja na Mama, ndugu yangu mkubwa Garth, na dada yangu Dawn, tukiwa tayari kusafiri kwenda kwenye kusanyiko la mwaka wa 1941 huko Sydney

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nikiwa na Judy na Kim nilipokuwa katika kazi ya mzunguko huko Queensland

[Picha katika ukurasa wa 15]

Baada ya mapacha wanne kuzaliwa, tulisaidiwa na wasichana wetu wakubwa wanne na kutaniko