Hamia kwenye habari

Kushoto: Wageni wakizunguka katika jumba la maonyesho. Katikati: Mwingilio wa jengo la La Modelo jijini Barcelona, nchini Hispania. Kulia: Nakala za barua ambazo ndugu mmoja alimwandikia mke wake alipokuwa gerezani

DESEMBA 5, 2023
HISPANIA

“Wamefungwa kwa Sababu ya Dhamiri Zao” Maonyesho ya Kipekee Kuwahusu Mashahidi wa Yehova Nchini Hispania

“Wamefungwa kwa Sababu ya Dhamiri Zao” Maonyesho ya Kipekee Kuwahusu Mashahidi wa Yehova Nchini Hispania

Wageni wakitembezwa ndani ya jengo lililokuwa gereza la La Modelo

Tangu Oktoba 14 hadi Desemba 16, 2023, kumekuwa na sehemu mpya yenye kichwa “Wamefungwa kwa Sababu ya Dhamiri Zao” katika jumba la makumbusho na kituo cha utamaduni la La Modelo jijini Barcelona, nchini Hispania, ambapo hapo awali palikuwa gereza la wahalifu. Maonyesho hayo yenye sehemu nne yamekusudiwa kuelimisha umma, kutia ndani maofisa wa serikali na wasomi, kuhusu imani yenye nguvu ya vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova waliokataa kuunga mkono upande wowote wa kisiasa.

Maonyesho hayo yanaeleza historia ya ndugu zetu ambao walifungwa gerezani nchini Hispania kuanzia miaka ya 1930 kwa sababu walikataa kujiunga na jeshi. Katika miaka ya 1960 na ya 1970 ndugu 1,000 hivi walikuwa gerezani, na ndugu 40 kati yao walikuwa katika gereza la La Modelo.

Sehemu inayoeleza kuwahusu ndugu waliokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri

Kuna vitu mbalimbali katika maonyesho hayo yanayosaidia watu kuelewa kwa nini Mashahidi wa Yehova wanakataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, na pia yanaonyesha vijana hao walipitia nini walipokuwa gerezani. Kwa sababu vijana hao walionyesha ujasiri kwa miaka mingi, mwaka wa 1984, serikali ya Hispania ilianza kutambua kisheria haki ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri.

Miguel Ángel Plaza ambaye ni profesa wa historia alipewa nafasi ya kuzungumza kwenye maonyesho hayo yalipofunguliwa. Alizungumza kuhusu baadhi ya Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa wamefungwa katika gereza la La Modelo. Naye alisema hivi kuwahusu: “Hakuna yeyote kati yao aliyewahi kukosoa au kusema jambo baya kuhusu maisha aliyoishi katika gereza la La Modelo—hata kuhusu walinzi wa gereza. Kila mmoja wao alikuwa na uso wenye shangwe alipokuwa akisimulia mambo aliyopitia alipokuwa gerezani.” Mmoja kati ya ndugu waliokuwa katika gereza hilo alikuwepo pia maonyesho hayo yalipofunguliwa. Ni Ndugu Fernando Trepat, naye alisema hivi: “Ingawa zaidi ya miaka 50 imepita, bado nina uhakika kwamba kanuni za Biblia zilinisaidia kufanya uamuzi mzuri. Hata leo hii, ningefanya uamuzi huohuo.”

Ndugu David Báidez, aliyekuwa msimamizi wa maonyesho hayo alisema hivi: “Ingawa maonyesho haya yanahusu mambo yaliyotokea zamani yanaweza kuwasaidia watu hata leo. Kwa sasa, kuna Mashahidi 200 hivi wa Yehova katika nchi mbalimbali ambao wamefungwa gerezani kwa sababu ya dhamiri zao zinazotegemea Biblia.”

Baadhi ya ndugu na dada waliokuwa wakiwatembeza wageni katika maonyesho ya La Modelo

Tunajivunia roho ya ushikamanifu na ya uvumilivu ambayo ndugu zetu walionyesha nchini Hispania kwa miaka mingi, na tunaendelea kusali kwa ajili ya wale ambao wamefungwa gerezani kwa sababu ya imani yao leo.​—Waebrania 13:3.