Hamia kwenye habari

KYRGYZSTAN

Maelezo Mafupi Kuhusu Kyrgyzstan

Maelezo Mafupi Kuhusu Kyrgyzstan

Mashahidi wa Yehova walianza utendaji wao nchini Kyrgyzstan tangu mwaka 1956 na kusajiliwa kisheria mwaka 1998. Ingawa kwa kipindi fulani wamenyanyaswa na kunyimwa uhuru wa ibada, hivi karibuni serikali imeendelea kulinda haki zao.

Novemba 2013, Baraza la Katiba la Mahakama Kuu liliamua kwa pamoja kwamba serikali ya Kyrgyzstan ilipaswa kurekebisha sehemu ya sheria ya utumishi wa badala ambayo haikufuata katiba. Mahakama za Kyrgyzstan zilitii agizo hilo la Baraza la Katiba, na hivyo tangu mwanzoni mwa mwaka 2014 wanaume Mashahidi hawahukumiwi kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. Juni 29, 2015, Kyrgyzstan ilirekebisha sheria inayohusu utumishi wa jeshi kwa kuwaruhusu wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri kufanya utumishi wa badala ambao hauko chini ya usimamizi wa jeshi.

Mwezi wa Septemba 2014, Baraza la Katiba la Mahakama Kuu liliwapa ushindi na uhuru wa kidini Mashahidi wa Yehova kwa kutangaza kwamba sehemu za sheria inayohusu dini ya mwaka wa 2008 zinapingana na katiba. Hata hivyo, Kamati ya Taifa ya Mahusiano ya Kidini imepuuza uamuzi wa Mahakama Kuu na imekataa kusajili mashirika ya kidini ya Mashahidi kusini mwa nchi. Kwa sababu ya kutosajiliwa, baadhi ya wenye mamlaka wameona utendaji wa Mashahidi kuwa si halali. Hata hivyo, kila mara Mashahidi wanapokutana na wenye mamlaka na kuwaeleza kuhusu shughuli zao za dini, mara nyingi wenye mamlaka huwaruhusu Mashahidi waendelee kukutana pamoja kwa ajili ya ibada na kuwahubiria majirani zao. Mashahidi wanatumaini kwamba serikali itafuata kikamili uamuzi wa Baraza la Katiba na kusajili mashirika ya kidini ya Mashahidi yaliyo kusini mwa Kyrgyzstan.