Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ULIMWENGU WENYE MISUKOSUKO

4 | Linda Tumaini Lako

4 | Linda Tumaini Lako

KWA NINI NI MUHIMU?

Mahangaiko kuhusu matatizo ya ulimwengu leo, yanaweza kuwaathiri watu kimwili na kihisia. Watu wengi walioathiriwa na matatizo hayo, hawana tumaini kwamba mambo yatakuwa sawa wakati ujao. Wanatendaje?

  • Baadhi yao hata wamekataa kufikiria kuhusu wakati ujao.

  • Wengine hutumia kileo au dawa za kulevya ili kuepuka kufikiria kuhusu matatizo yao.

  • Baadhi ya watu wamefikia mkataa kwamba ni afadhali wafe kuliko kuwa hai. Hata wamesema kwamba hakuna faida ya kuishi.

Unachopaswa Kujua

  • Huenda baadhi ya matatizo unayokabili ni ya muda mfupi na mambo yanaweza kuwa bora bila wewe kutarajia.

  • Hata kama hali yako haitabadilika, unaweza kufanya mambo yatakayokusaidia kukabiliana na hali hiyo.

  • Biblia inaahidi suluhisho la kudumu la matatizo ya wanadamu.

Unachoweza Kufanya Sasa

Biblia inasema hivi: “Msihangaike kamwe kuhusu kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Kila siku ina matatizo yake ya kutosha.”​—Mathayo 6:34.

Shughulikia matatizo ya leo. Usiruhusu mahangaiko ya kesho yakuzuie kutimiza majukumu yako ya leo.

Kuhofia mambo mabaya ambayo huenda yakatokea wakati ujao, kutakuongezea mkazo na kudhoofisha tumaini lako kwamba mambo yatakuwa mazuri wakati ujao.

Biblia Inatoa Tumaini la Kweli

Zamani, mtunga-zaburi alisali hivi kwa Mungu: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru ya njia yangu.” (Zaburi 119:105) Ona jinsi Neno la Mungu, Biblia, lilivyo kama taa:

Taa hutusaidia kutambua mahali pa kukanyaga tunapotembea usiku. Vivyo hivyo, Biblia ina ushauri wenye hekima unaoweza kutuongoza tunapohitaji kufanya uamuzi mgumu.

Taa inaweza kutusaidia kujua njia tunayopita ili tuweze kuona kilicho mbele yetu. Kwa njia hiyohiyo, Biblia inaweza kutusaidia kuona mambo yatakayotokea wakati ujao.