Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye Mafanikio

Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye Mafanikio

Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye Mafanikio

NDOA inaweza kufananishwa na safari ndefu yenye matukio yasiyotazamiwa, mengine yenye kupendeza na mengine yenye kuumiza. Hali zisizotazamiwa zinaweza kutokeza vizuizi visivyotarajiwa, vingine vikionekana kuwa vikubwa sana. Hata hivyo, watu wengi humaliza safari hiyo kwa furaha na mafanikio, wakiwa wamekabili matatizo madogo tu. Kwa kweli, mafanikio katika ndoa hayapimwi kwa panda shuka za safari bali yanapimwa kwa jinsi wenzi wanavyoshughulikia hali hizo.

Unafikiri ni nini kinachoweza kufanya safari ya ndoa ifanikiwe zaidi na iwe yenye kufurahisha? Wenzi wengi wanaona uhitaji wa kuwa na ‘ramani ya ndoa’ ili iwaelekeze njiani. “Ramani” inayotegemeka na yenye mamlaka kuhusu ndoa imeandaliwa na Mwanzilishi wa ndoa—Yehova Mungu. Hata hivyo, Neno lake lililoongozwa na roho, Biblia Takatifu, si hirizi. Badala yake, lina mwelekezo unaofaa ambao wenzi waliooana wanapaswa kufuata ili ndoa yao ifanikiwe.—Zaburi 119:105; Waefeso 5:21-33; 2 Timotheo 3:16.

Acheni tuone baadhi ya alama za Kimaandiko za kuonyesha njia, yaani, kanuni muhimu za Biblia ambazo zinaweza kukuongoza katika safari ya ndoa yenye furaha na mafanikio.

Ione ndoa kuwa takatifu. “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:6) Muumba alianzisha mpango wa ndoa alipomleta Hawa kwa mwanamume wa kwanza, Adamu. (Mwanzo 2:21-24) Kristo Yesu, ambaye alishuhudia tukio hilo alipokuwa mbinguni alithibitisha kwamba muungano wa Adamu na Hawa katika ndoa ulipaswa kudumu. Alisema: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:4-6.

Kwa kusema “kile ambacho Mungu ameunganisha,” Yesu hakuwa akidokeza kwamba Mungu hupanga ndoa mbinguni. Badala yake, alikuwa akithibitisha kwamba uhusiano wa ndoa ulianzishwa na Mungu mwenyewe na hivyo ulipaswa kuonwa kuwa mtakatifu. *

Bila shaka, waume na wake hawangependa ‘kuunganishwa’ katika uhusiano usio na upendo. Badala yake, wanataka kufurahia ndoa yenye kuridhisha itakayowaimarisha. Wanaweza ‘kuunganishwa’ kwa furaha ikiwa watafuata mashauri ya Muumba yanayopatikana katika Biblia.

Kwa sababu sisi sote si wakamilifu, hatuwezi kuepuka kutoelewana na kutopatana. Hata hivyo mara nyingi, ndoa yenye mafanikio haitegemei kufaana kwa wenzi wa ndoa, bali inategemea jinsi wanavyokabiliana na mambo ambayo hawapatani. Hivyo, mbinu moja muhimu sana katika ndoa ni uwezo wa kusuluhisha mambo kwa upendo, kwa kuwa upendo “huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili.”—Wakolosai 3:14, Biblia Habari Njema.

Zungumza kwa heshima. “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Wachunguzi wamegundua kwamba mazungumzo mengi huisha vile yalivyoanza. Kwa hiyo, ikiwa mazungumzo yanaanza kwa heshima, kuna uwezekano mkubwa kwamba yatamalizika vivyo hivyo. Kwa upande mwingine, unajua jinsi unavyoumia mpendwa anapokuambia jambo bila kufikiri. Hivyo, sali na ujitahidi kuzungumza kwa staha, heshima, na upendo. (Waefeso 4:31) “Hata ingawa kila mmoja huona udhaifu wa mwenzake,” anaeleza Haruko, * mwanamke Mjapani ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 44, “tunajitahidi kuheshimiana kwa maneno na mtazamo. Hilo limetusaidia kuwa na ndoa yenye mafanikio.”

Sitawisha fadhili na huruma. “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo.” (Waefeso 4:32) Kunapokuwa na ugomvi mkali, mara nyingi mwenzi mmoja akikasirika yule mwingine hukasirika pia. Huko Ujerumani, Annette, ambaye amekuwa katika ndoa yenye furaha kwa miaka 34 anakiri hivi: “Si rahisi kuwa mtulivu chini ya mfadhaiko—inaelekea utasema mambo yatakayomkasirisha mwenzi wako, na kufanya hali iwe mbaya hata zaidi.” Hata hivyo, kwa kujitahidi kuwa mwenye fadhili na huruma, unaweza kuchangia sana katika kunyoosha njia ya kupata ndoa yenye amani.

Onyesha unyenyekevu. ‘Usifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili ukiwaona wengine kuwa ni bora.’ (Wafilipi 2:3) Ugomvi mwingi hutokea kwa sababu badala ya kujinyenyekeza na kutafuta njia za kuboresha hali, kiburi huwafanya watu walaumu wenzi wao matatizo yanapotokea katika ndoa. Unyenyekevu wa akili unaweza kukusaidia usisisitize kwamba wewe ndiye uko sawa ugomvi unapotokea.

Usiudhike haraka. “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako.” (Mhubiri 7:9) Jaribu kuepuka mwelekeo wa kupinga maoni ya mwenzi wako au kujitetea haraka mwenzi wako akikuuliza kuhusu jambo ulilosema au kufanya. Badala yake, sikiliza maoni ya mwenzi wako. Fikiria kwa uangalifu kabla ya kujibu. Watu wengi hujifunza wakiwa wamechelewa mno kwamba kuwa na uhusiano wenye upendo na wenzi wao ni muhimu kuliko kushinda mabishano.

Jua wakati wa kukaa kimya. ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Bila shaka, mawasiliano mazuri ni mojawapo ya ishara muhimu sana katika barabara inayoelekeza kwenye ndoa yenye furaha. Kwa nini basi Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya”? (Mhubiri 3:7) Huenda huo ukawa wakati wa kusikiliza kwa makini ili uelewe anachosema mwenzi wako, na hiyo ni sehemu muhimu ya mawasiliano inayotia ndani kujua hisia za mwenzi wako wa ndoa na kwa nini anahisi hivyo.

Onyesha hisia-mwenzi unaposikiliza. “Shangilieni pamoja na watu wanaoshangilia; lieni pamoja na watu wanaolia.” (Waroma 12:15) Hisia-mwenzi ni muhimu ili kuwasiliana inavyofaa kwa sababu inakuwezesha kuhisi hisia za ndani kabisa za mwenzi wako. Sifa hiyo inawezesha kuwe na hali ambayo maoni na hisia za kila mmoja zinaheshimiwa. Nella kutoka Brazili ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 32 anasema hivi: “Tunapozungumzia matatizo yetu, mimi husikiliza kwa makini ili nielewe mawazo na hisia za Manuel.” Mwenzi wako anapozungumza, huo ni “wakati wa kukaa kimya” na kumsikiliza ukionyesha hisia-mwenzi.

Uwe na zoea la kuonyesha uthamini. “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.” (Wakolosai 3:15) Waume na wake katika ndoa imara huhakikisha kwamba wenzi wao wanajua jinsi wanavyowathamini. Hata hivyo, kwa sababu ya pilka-pilka za kila siku katika ndoa, watu fulani wamepuuza sehemu hiyo muhimu ya mawasiliano na kudhani kwamba wenzi wao wanajua wanathaminiwa. “Wenzi wengi,” anasema Dakt. Ellen Wachtel, “wangeweza kuonyeshana uthamini ikiwa wangekumbuka kufanya hivyo.”

Wake hasa wanahitaji kuhakikishiwa kwa upendo na kuonyeshwa na waume wao kwamba wanathaminiwa. Waume, mnaweza kufanya mengi kuboresha ndoa yenu na hali njema ya wake wenu na yenu wenyewe kwa kuwa na zoea la kuwapongeza wake wenu kwa sababu ya matendo mazuri na sifa zao.

Ni muhimu kumhakikishia hivyo kwa maneno na kwa matendo. Mume, unapombusu mke wako, kumgusa kwa wororo, na kutabasamu kwa uchangamfu, mambo hayo yanatimiza mengi zaidi ya kumwambia “nakupenda.” Kufanya hivyo kunamhakikishia kwamba yeye ni mwenye thamani kwako na unamhitaji. Mpigie simu au umwandikie ujumbe mfupi kwa simu ukimwambia, “ninakukosa” au ukimwuliza “Siku yako inaendeleaje?” Ikiwa umeacha mazoea hayo ambayo ulikuwa nayo mlipokuwa mkichumbiana, ingefaa uanze tena. Endelea kutafuta ni nini kinachomgusa moyo.

Maneno haya ya mama ya Mfalme Lemueli wa Israeli la kale yanafaa: “Mumewe huimba sifa zake. Husema, ‘Wanawake wengi wametenda mambo ya ajabu, lakini wewe umewashinda wote.’” (Methali 31:1, 28, 29, BHN) Wewe ulimsifu mke wako lini mara ya mwisho? Au ikiwa wewe ni mke, ulimsifu mume wako lini?

Uwe mwenye haraka kusamehe. “Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Ukiwa katika ndoa, wewe na mwenzi wako hamwezi kuepuka kufanya makosa. Hivyo, kuwa tayari kusamehe ni muhimu. Clive na Monica, huko Afrika Kusini, ambao wameoana kwa miaka 43, wameona shauri hili la Biblia kuwa lenye kusaidia sana. Clive anaeleza hivi: “Sisi hujaribu kutumia kanuni inayopatikana katika Waefeso 4:26, nasi hujaribu kusameheana haraka, kwa kuwa tunajua kwamba hilo humpendeza Mungu. Baada ya hapo, sisi hulala vizuri kwa kuwa tuna dhamiri safi.”

Methali ya kale inasema hivi kwa hekima: ‘Ni jambo lenye kupendeza kupita kosa.’ (Methali 19:11) Annette, aliyetajwa awali, anakubaliana na hilo, naye anaongezea: “Hamwezi kuwa na ndoa nzuri ikiwa hamsameheani.” Anaeleza sababu: “Msiposameheana, mtakuwa na kinyongo na kutoaminiana, na mambo hayo ni sumu kwa ndoa. Mnaposameheana, kifungo cha ndoa huimarishwa na mnakuwa na uhusiano wa karibu sana.”

Unapomuumiza mwenzi wako kihisia, usikate kauli kwamba atakusamehe na kusahau. Mara nyingi, kufanya amani kunahusisha mojawapo ya mambo magumu kwa wenzi wa ndoa: Kukubali kwamba umefanya makosa. Tafuta njia za kusema hivi kwa unyenyekevu: “Naomba radhi, mpenzi. Nilikosea.” Kuomba msamaha kwa unyenyekevu kutafanya uheshimiwe, uaminiwe, na uwe na amani ya akili.

Uwe mwaminifu kwa mwenzi wako na kwa ndoa yako. “Wao [mume na mke] si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:6) Wewe na mwenzi wako mliweka nadhiri nzito mbele za Mungu na watu kwamba mtaishi pamoja, chini ya hali zozote zile. * Hata hivyo, kutimiza wajibu katika ndoa hakuhusishi kutimiza matakwa ya kisheria tu. Badala yake, mtu anapaswa kuchochewa na upendo wa kutoka moyoni, na hilo litaonyesha kwamba anamheshimu na kumstahi Mungu na pia mwenzi wake. Kwa hiyo, usidhoofishe ndoa yako takatifu kwa kucheza-cheza na wengine kimapenzi; pendezwa kimahaba na mwenzi wako tu.—Mathayo 5:28.

Kujidhabihu kunaimarisha ushikamanifu. ‘Endelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yako mwenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Kutanguliza mahitaji na mapendezi ya mwenzi wako ni njia moja ya kuimarisha ushikamanifu wako. Premji, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 20, humsaidia kazi za nyumbani mke wake ambaye anafanya kazi ya kuajiriwa. “Mimi humsaidia Rita kupika, kusafisha, na kazi nyingine ili awe na wakati na nguvu za kufanya mambo anayopenda.”

Jitihada Zinathawabisha

Nyakati nyingine, huenda kazi ngumu inayohusika ili kuwa na ndoa yenye furaha ikafanya watu fulani watake kukata tamaa. Hata hivyo, usiache matatizo yakufanye uache kutimiza wajibu au utupilie mbali jitihada ambazo umefanya kufikia sasa kufanikisha ndoa yako, yaani, usikatize safari yako ya kuwa na ndoa yenye mafanikio.

“Ukijitahidi vilivyo na kuonyesha kwamba unataka ndoa yako ifanikiwe, utapata baraka za Yehova,” anasema Sid, ambaye ndoa yake imefanikiwa kwa miaka 33. Mkitegemezana kwa ushikamanifu nyakati za shida na mkifurahia pamoja nyakati za shangwe mtadumu katika safari yenye kuridhisha ya kuwa na ndoa yenye mafanikio.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Yesu alisema kwamba msingi pekee wa kuvunja ndoa na kuwa huru kuoa au kuolewa tena ni uasherati, yaani, ngono nje ya ndoa.—Mathayo 19:9.

^ fu. 9 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 22 Biblia inampa mwenzi asiye na hatia haki ya kuamua ikiwa atamtaliki mwenzi aliyefanya uzinzi. (Mathayo 19:9) Ona makala “Maoni ya Biblia: Uzinzi—Kusamehe au Kutosamehe?” katika Amkeni! la Agosti 8, 1995 (8/8/1995).

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Biblia ni kama ramani ya kutuongoza katika safari ya ndoa

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Mnapohitaji kuzungumzia tatizo fulani

Pangeni kufanya hivyo wakati hamjachoka.

Epukeni kuchambuana na muwe na mtazamo unaofaa.

Epuka kumkatiza mwenzako anapoongea; kila mmoja awe na zamu ya kusikiliza na kuongea.

Tambua hisia za mwenzi wako.

Onyeshaneni hisia-mwenzi, hata msipokubaliana.

Muwe na usawaziko na tayari kubadilikana.

Omba msamaha kwa unyenyekevu unapokosea.

Onyeshaneni uthamini na upendo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

Ili ndoa ifanikiwe

Zingatia kweli za Biblia ambazo huimarisha ndoa.

Tafuta wakati kwa ajili ya ndoa na mwenzi wako.

Uwe mchangamfu, mwenye upendo, na urafiki.

Uwe mwenye kuaminika na mshikamanifu.

Onyesha fadhili na heshima.

Saidia kazi za nyumbani.

Jitahidi kuwa na mazungumzo yenye kufurahisha.

Iweni na ucheshi na tafrija pamoja.

Endeleeni kujitahidi kuimarisha ndoa yenu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Mambo ya kutafakari kibinafsi

Ninahitaji kufanyia kazi nini katika ndoa yangu?

Nitachukua hatua gani kufanya hivyo?