Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uepuke Kuwasiliana na Pepo?

Kwa Nini Uepuke Kuwasiliana na Pepo?

Maoni ya Biblia

Kwa Nini Uepuke Kuwasiliana na Pepo?

KATIKA nchi moja barani Asia, umati unasherehekea sikukuu ya kuheshimu pepo au mashetani. Sherehe hiyo inafikia kilele wanawake wawili wanapochaguliwa kwa ajili ya sherehe ya kuingiwa na mashetani. Macho yao yanaingia ndani, kisha wanaanza kutetemeka kana kwamba wamepigwa na umeme.

Nchini Puerto Riko, mtu anayewasiliana na pepo (santero) anajaribu kuwasiliana na pepo anayeitwa Changó, mungu wa ngurumo. Yule anayewasiliana na pepo anaeleza maono fulani, na wote katika chumba wanaanza kutetemeka kana kwamba wameingiwa na mashetani.

Katika nchi nyingi, ni jambo la kawaida kujihusisha na uchawi. Watu wengi zaidi wanaamini mambo yanayopita uwezo wa mwanadamu na wanavutiwa nayo. Vitabu, michezo, vipindi vya televisheni, na sinema ambazo huonyesha mashetani, uchawi, na matukio yasiyo ya kawaida zimeongezeka sana kuliko zamani.

Ingawa hivyo, Biblia inafundisha kwamba kujihusisha katika uchawi wowote ni kuwasiliana na pepo. Kuwasiliana na pepo si jambo la kujifurahisha tu lisilo na madhara yoyote wala si uvumbuzi wa mambo yasiyojulikana. Ni kuzungumza na mashetani, malaika waovu waliomwasi Mungu.—Ufunuo 12:9, 12.

Kwa kweli, mashetani huyatumia mazoea ya kuwasiliana na pepo kama vile mvuvi anavyotumia chambo kwenye ndoana. Mvuvi hutumia vyambo vya aina mbalimbali ili kunasa samaki wa namna mbalimbali. Vivyo hivyo, mashetani hutumia njia mbalimbali za kuwasiliana na pepo ili kuwanasa watu wa namna zote. Kiongozi wa mashetani anatajwa kuwa “mungu wa mfumo huu [mwovu] wa mambo.” Amefaulu kuzipofusha akili za wasioamini ili wasione ukweli wa Neno la Mungu na kusudi lake.—2 Wakorintho 4:4.

Kuwasiliana na Pepo Kunaongoza Wapi?

Lengo la mashetani ni rahisi: Wanataka kutukengeusha na kutupotosha ili tusiwe na uhusiano wa karibu na Muumba wetu. Wanafanya watu wasitii matakwa ya uadilifu ya Mungu, iwe wanajua au hawajui. Kwa hiyo, wale wanaowasiliana na pepo hukosa kibali cha Mungu, hawana tumaini, na hatimaye wataharibiwa.—Ufunuo 21:8.

Luis kutoka Puerto Riko anasema hivi: “Tangu nilipokuwa mtoto, familia yetu iliwasiliana na pepo. Hiyo ilikuwa sehemu ya dini ya familia na njia yetu ya maisha. Nilidhani kwamba uwezo wangu wa kuona wakati ujao na kusoma kadi za ubashiri ulikuwa jambo la kawaida. Mara nyingi, niliweza kuchagua nambari za ushindi za bahati nasibu na kuwasaidia watu kushinda pesa. Hata hivyo, uwezo huo ulikuwa tu mbinu ya kunikengeusha ili nisiijue Biblia na kusitawisha uhusiano na Mungu.”—Yohana 17:3.

Watu wengi hufikiri kwamba kujihusisha na ulimwengu wa mashetani hakuna madhara yoyote, na hata kunaweza kunufaisha. Wao huhisi kuna pepo wazuri au wanadai kwamba kuwasiliana na pepo kunaweza kuwapa ujuzi zaidi, mali, au furaha. Hilo si kweli hata kidogo. “Sikuzote utapata hasara,” anasema Luis.

Kijana anayeitwa Chad alianza kuwa na maono yenye kuogopesha na mfadhaiko wa kuamshwa kila mara alipolala. “Mashetani walianza kunisumbua na kunitesa kila usiku,” anasema. Tunawezaje kulindwa dhidi ya mateso kama hayo?

Jinsi ya Kupata Ulinzi

Ili kujilinda, tunapaswa kuepuka kitu chochote kinachohusiana na kuwasiliana na pepo. (Wagalatia 5:19-21) Hivyo, Yehova Mungu anawaamuru watumishi wake waepuke mazoea yafuatayo: “Asipatikane ndani yako yeyote . . . anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu au yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Kupatana na maneno hayo, wengi wamechukua hatua ili kujilinda kwa kuharibu vitabu au kitu chochote kinachohusiana na kuwasiliana na pepo. Ken, ambaye aliacha kuwasiliana na pepo anasema, “Nilikagua vitu vyangu vyote na kuharibu kitu chochote nilichoona kuwa kibaya.”—Ona Matendo 19:19, 20.

Ulinzi mkubwa zaidi ni kusitawisha uhusiano wa karibu na Mungu wa kweli, Yehova. Ona hatua tunayopaswa kuchukua ambayo inatajwa kwenye andiko la Yakobo 4:7, 8: “Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Safisheni mikono yenu, ninyi watenda-dhambi, na takaseni mioyo yenu, ninyi wenye kusitasita.”

Yehova Mungu anawaelimisha na kuwalinda wale wanaomkaribia. Wao ‘hawakosi kuzijua mbinu za Shetani’ au hawadanganywi na jinsi anavyojibadili-badili. (2 Wakorintho 2:11; 11:14) Pia, Yehova ni Mweza-Yote. Watu wanapomwita Yehova kwa imani, yeye atawaweka huru kutokana na usumbufu wa mashetani. Chad, aliyetajwa mapema anasema, “Kujua chanzo cha mashambulizi na kumwita Yehova Mungu ili anilinde kutokana na uvutano wao kuliyakomesha.”—Zaburi 91:1, 2.

Ni wazi kwamba watu wenye mioyo minyoofu wanaweza kufurahia ulinzi wa Mungu sasa wakijua kwamba hivi karibuni, mashetani wote na wale wanaokubali kuwa chini ya uvutano wao wataharibiwa. Hebu wazia shangwe na amani itakayokuwa duniani wakati wanadamu watakapowekwa huru kutokana na madhara ya kuwasiliana na pepo!—Isaya 11:9; Ufunuo 22:15.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Mkristo anapaswa kuepuka mazoea gani ya kuwasiliana na pepo?—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ufunuo 21:8.

▪ Ni nani anayewachochea watu wawasiliane na pepo?—2 Wakorintho 2:11; 11:14; Ufunuo 12:9, 12.

▪ Tunaweza kujilindaje dhidi ya mashetani?—Yakobo 4:7, 8.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa kweli, mashetani huyatumia mazoea ya kuwasiliana na pepo kama vile mvuvi anavyotumia chambo kwenye ndoana