Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Latoa Msaada Usiotazamiwa

Latoa Msaada Usiotazamiwa

Latoa Msaada Usiotazamiwa

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI BENIN

▪ Noël, mwenye umri wa miaka 23 alipoamua kuacha shule na kuwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, watu wake wa ukoo walifikiri kwamba hangeweza kupata pesa za kujitegemeza. Ni kweli kwamba ilikuwa vigumu kwake kupata kazi inayofaa ambayo si ya wakati wote. Hivyo, gazeti Amkeni! lilipochapisha makala yenye kichwa “Mbinu Tano za Kutafuta Kazi,” Noël aliisoma kwa makini mara kadhaa. * Je, ilimsaidia? Ndiyo, lakini kwa njia ambayo hakutarajia.

Msimamizi wa shule moja ya kibinafsi alimwona Noël akihubiri nyumba kwa nyumba na kumwuliza ikiwa yeye ni mmoja Mashahidi wa Yehova. Msimamizi huyo alihitaji mwalimu, na kwa sababu alikuwa ameona kwamba Mashahidi wa Yehova hufundisha vizuri, alimwuliza Noël kama alimfahamu mtu yeyote ambaye angetaka kazi hiyo. Noël alipojibu la, msimamizi huyo akamwuliza, “Vipi wewe?”

Noël hakuwa amewahi kufanya kazi ya ualimu, na nyakati nyingine alikuwa na kigugumizi. Hilo lilikuwa tatizo huko Benin kwa sababu baraza la elimu liliwataka walimu wafanye mtihani wa kuthibitisha kwamba hawana kigugumizi. Msimamizi huyo alimwambia hivi Noël: “Tafuta cheti kwanza kisha nitakuajiri.”

Noël alikuwa amefanya maendeleo mazuri katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambayo imekusudiwa kuboresha uwezo wa mtu wa kusema mbele ya watu. Shule hiyo hufanywa kila juma katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Hata alitoa hotuba za watu wote katika kutaniko lao. Lakini, alikuwa na wasiwasi alipoenda kufanya mtihani huo.

Mtahini alimpa gazeti na kumwomba asome kwa sauti fungu lililotiwa alama nyekundu. Noël alishangaa alipoona makala yenye kichwa “Mbinu Tano za Kutafuta Kazi.” Alisoma fungu hilo kwa ufasaha na akapata cheti.

Baadaye mtahini huyo alisema kuwa yeye husoma magazeti ya Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida. Alieleza hivi: “Magazeti hayo yanatoa habari muhimu na yameandikwa kwa njia nzuri sana hivi kwamba mimi huyatumia kwa ajili ya mitihani.”

Noël alianza kufundisha na msimamizi huyo alitaka kumwajiri tena mwaka uliofuata, lakini Noël alikuwa na mipango mingine. Alikuwa amealikwa afanye kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ambako anatumika sasa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona toleo la Amkeni! la Julai 8, 2005 (8/7/2005), ukurasa wa 4-9.