Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku ya Hukumu Ni Nini?

Siku ya Hukumu Ni Nini?

Maoni ya Biblia

Siku ya Hukumu Ni Nini?

Biblia inasema kuwa Mungu “ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa.” (Matendo 17:31) Watu wengi hawapendi wazo la kuja kuhukumiwa kwa njia yoyote ile. Je, hivyo ndivyo unavyohisi?

IKIWA unahisi hivyo, unaweza kufarijika kujua kuwa Siku ya Hukumu ni mpango wenye upendo utakaowaletea wanadamu baraka nyingi—kutia ndani wale ambao wamekufa. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Siku ya Hukumu ina umuhimu gani? Ni nini kitakachotokea “siku” hiyo?

Kwa Nini Siku ya Hukumu Ni Muhimu?

Mungu alipowaweka wanadamu duniani hakukusudia pawe mahali pa kuwahukumu wanadamu ili wakaishi mahali pengine baadaye. Aliwaumba wanadamu waishi milele duniani. Wanadamu wa kwanza walimwasi Mungu ingawa walikuwa wakamilifu kimwili na kiakili. Kwa sababu hiyo, walipoteza tumaini lao la uzima wa milele na pia wakaleta dhambi na kifo kwa uzao wao wote.—Mwanzo 2:15-17; Waroma 5:12.

Siku ya Hukumu itakuchukua muda wa miaka elfu moja ambapo wanadamu watakuwa na nafasi ya kupata kile Adamu na Hawa walipoteza. * Ona kwamba andiko la Matendo 17:31 lililonukuliwa hapo juu linasema kwamba Siku ya Hukumu itawaathiri wale wanaoishi juu ya “dunia inayokaliwa.” Wale wanaohukumiwa kuwa wanastahili, wataishi juu ya dunia na kufurahia uzima wa milele wakiwa wakamilifu. (Ufunuo 21:3, 4) Kwa hiyo, Siku ya Hukumu inasaidia kutimiza kusudi la awali la Mungu kwa wanadamu na dunia.

Hakimu aliyewekwa rasmi na Mungu ni Kristo Yesu. Biblia inasema kuwa Yesu ‘atawahukumu walio hai na wafu.’ (2 Timotheo 4:1) Hawa “walio hai” watakaohukumiwa ni akina nani? Wafu watafufuliwaje katika “dunia inayokaliwa”?

Yesu Anawahukumu “Walio hai”

Sasa tumekaribia ule mwisho uliotabiriwa wa huu mfumo wa mambo, wakati ambapo Mungu ataharibu kila sehemu ya jamii ya wanadamu yenye ufisadi na kuwaondoa waovu. Waokokaji wa mwisho wa mfumo huu ndio “walio hai” ambao watahukumiwa.—Ufunuo 7:9-14; 19:11-16.

Katika kipindi hicho cha hukumu ambacho kitachukua muda wa miaka 1,000, Kristo Yesu na wanaume na wanawake 144,000 watakaokuwa wamefufuliwa ili kwenda mbinguni watatawala juu ya dunia. Watatumikia wakiwa wafalme na makuhani, wakiwasaidia watu wafaidike na dhabihu ya ukombozi ya Yesu na kuwasaidia wanadamu waadilifu wafikie kuwa wakamilifu kimwili na kiakili.—Ufunuo 5:10; 14:1-4; 20:4-6.

Katika Siku ya Hukumu, Shetani na mashetani wake watafungwa ili wasiwe na uvutano wowote juu ya wanadamu. (Ufunuo 20:1-3) Hata hivyo, mwishoni mwa Siku ya Hukumu, Shetani ataruhusiwa ajaribu ushikamanifu wa kila mwanadamu aliye hai. Wale watakaobaki wakiwa washikamanifu kwa Mungu watakuwa wamepita jaribu ambalo Adamu na Hawa walianguka. Watahukumiwa kuwa wanastahili kupata uzima wa milele katika dunia iliyorudishwa kuwa Paradiso. Wale watakaochagua kumwasi Mungu wataharibiwa kabisa pamoja na Shetani na mashetani wake.—Ufunuo 20:7-9.

Kuwahukumu “Wafu”

Biblia inasema kwamba wafu “watasimama” katika Siku ya Hukumu. (Mathayo 12:41) Yesu alisema kuwa “saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28, 29) Hilo halizungumzi kuhusu nafsi zilizotenganishwa na miili ya wale waliokufa. Wafu hawajui lolote kamwe na pia hawana nafsi inayoendelea kuishi baada ya kifo. (Mhubiri 9:5; Yohana 11:11-14, 23, 24) Yesu atawafufua wale waliolala katika kifo ili waishi tena duniani.

Je, wafu watahukumiwa kulingana na kile walichofanya kabla ya kufa? La. Biblia inafundisha kwamba “yeye ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” (Waroma 6:7) Kwa hiyo, kama tu wale watakaookoka mwisho wa huu mfumo wa mambo, wale watakaofufuliwa tena ili waishi juu ya dunia watahukumiwa “kulingana na matendo yao” katika Siku ya Hukumu. (Ufunuo 20:12, 13) Ikitegemea matendo yao, watapata ufufuo unaowaletea uzima wa milele au ufufuo wa uharibifu. Wengi watakaofufuliwa, watajifunza kwa mara ya kwanza kumhusu Yehova Mungu na matakwa yake. Watakuwa na nafasi ya kuishi kupatana na mapenzi ya Mungu na kupata uzima wa milele duniani.

Hakuna Sababu ya Kuogopa

Siku ya Hukumu haitakuwa tu wakati wa kupokea maagizo kutoka kwa Mungu, bali pia utakuwa wakati wa wale walio hai kutii yale waliyojifunza na kufurahia baraka zitakazotokana na utii wao. Hebu wazia furaha ya kuungana tena na wapendwa wetu watakaofufuliwa na kufanywa wakamilifu pamoja nao!

Mungu atamruhusu Shetani ajaribu ushikamanifu wa wanadamu mwishoni mwa Siku ya Hukumu. Lakini hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi wala kuogopa. Kufikia mwisho wa Siku ya Hukumu, wote walio hai watakuwa wamejihami vya kutosha kwa ajili ya jaribu la mwisho. Hivyo, Siku ya Hukumu itakuwa sehemu ya kutimizwa kwa kusudi la Mungu la kuondoa madhara yote yaliyosababishwa na uasi uliotokea katika shamba la Edeni.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Katika Biblia neno “siku” linaweza kumaanisha kipindi cha wakati chenye urefu tofauti-tofauti. Kwa mfano, ona Mwanzo 2:4.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Siku ya Hukumu ni nini?—Matendo 17:31.

● Ni nani watakaohukumiwa?—2 Timotheo 4:1.

● Siku ya Hukumu itakuwa na urefu gani?—Ufunuo 20:4-6.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Hebu wazia furaha ya kuungana tena na wapendwa wetu watakaofufuliwa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Chini ya utawala wa Kristo, wafu watafufuliwa na kuishi kwenye dunia paradiso