Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahakama ya Hispania Yampa Mama Haki ya Kuwalea Watoto

Mahakama ya Hispania Yampa Mama Haki ya Kuwalea Watoto

Mahakama ya Hispania Yampa Mama Haki ya Kuwalea Watoto

● Ikiwa ungeambiwa wewe si mzazi mzuri ungehisi namna gani? Vipi ikiwa mtu angedai kuwa watoto wako hawajui jinsi ya kushirikiana na watu, hawawezi kutofautisha kati ya mema na mabaya, na hawana akili kama ya watoto wengine—yote hayo kwa sababu yako?

Rosa López, mama mwenye watoto wawili kutoka Hispania, alikabiliwa na mashtaka kama hayo wakati mwanamume aliyekuwa mume wake alipotaka kupata haki ya kisheria ya kulea watoto wao. Rosa ni Shahidi wa Yehova, na mwanamume huyo alisema kuwa imani ya Rosa ilikuwa ikiathiri maisha, masomo, na uwezo wa kuamua mambo ya msingi maishani mwa binti zao. Wakati mahakama ya chini ilipokataa madai yake, mwanamume huyo aliamua kukata rufaa katika mahakama ya mkoa.

Katika kesi kama hiyo ya malezi, mahakama hujaribu kutopendelea upande wowote kwa kufanya uchunguzi unaofaa, pia haijihusishi katika mabishano ya kidini, wala kutilia shaka imani ya mtu yeyote. Badala yake, mahakama hukazia fikira mambo kama: Je, masilahi ya mtoto yanatimizwa? Je, mzazi ambaye amepewa haki ya kumlea mtoto ana uvutano mbaya? Ni mzazi yupi anayeweza kutimiza mahitaji ya mtoto kwa njia inayofaa zaidi?

Ili kushughulikia kesi ya Rosa, mahakama ilichagua mwanasaikolojia aliyewahoji watoto hao na pia wazazi wao. Kulikuwa na matokeo gani? Mwanasaikolojia huyo alitambua kuwa ingawa watoto hao walikuwa wameishi na mama yao kwa miaka sita, walikuwa sawa katika nyanja zote za maisha—iwe ni shuleni, kushirikiana na watu, na katika familia. Kutokana na uthibitisho wa mwanasaikolojia huyo na ushahidi uliotolewa na wazazi, hakimu alisema kwamba hakupata uthibitisho wowote unaonyesha kwamba “watoto hao walikuwa wameathiriwa vibaya kihisia na katika maisha yao ya kila siku kwa sababu walilelewa kati ya Mashahidi wa Yehova.” Pia aliamua kwamba madai yaliyotolewa na mwanamume huyo “hayakuwa na msingi wowote wala hayakuwa ya kweli.”

Kwa sababu ya ubaguzi wa kidini au habari zisizo za kweli, watu fulani hufikiri kwamba watoto wa Mashahidi wa Yehova wananyimwa malezi ya “kawaida.” Lakini, watoto waliolelewa kulingana na kanuni za Biblia hawateswi. Badala yake, wanasaidiwa kuwa watu wenye usawaziko, wenye kujali, na wenye ustadi na mazoea ambayo yatawasaidia baadaye maishani.—Waefeso 6:4; 2 Timotheo 3:15-17.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Rosa López alipewa haki ya kuwalea binti zake wawili