Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Kutafakari

Kutafakari

Kunamaanisha nini?

“Nitautafakari utendaji wako wote, nami nitajishughulisha mwenyewe na matendo yako.”​—Zaburi 77:12.

WATU HUSEMA NINI?

Watu hutafakari kwa njia nyingi, baadhi ya njia hizo zilianza zamani katika dini za Mashariki. “Lazima akili iwe tupu ili ifikirie vizuri,” akasema mwandikaji mmoja kuhusiana na kutafakari. Maneno yake yanaonyesha wazo la kukazia fikira maneno au picha fulani ili kupata amani ya moyoni, utulivu wa kiakili, na ujuzi wa kiroho.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inaonyesha kwamba kutafakari ni jambo muhimu sana. (1 Timotheo 4:15) Hata hivyo, kutafakari kunakotajwa katika Biblia hakumaanishi kuondoa mawazo akilini au kurudia maneno fulani ambayo huitwa mantra. Badala yake, kutafakari kunakotajwa katika Biblia kunahusisha kufikiria kwa makini kuhusu mambo yanayofaa kama vile sifa, viwango, na uumbaji wa Mungu. Mtumishi mmoja mwaminifu wa Mungu alisali hivi: “Nimetafakari juu ya utendaji wako wote; . . . Niliendelea kuhangaikia kazi ya mikono yako mwenyewe.” (Zaburi 143:5) Pia, alisema: “[Nina]kukumbuka kitandani mwangu, wakati wa makesha ya usiku natafakari juu yako.”—Zaburi 63:6.

 Kutafakari kunawezaje kukusaidia?

“Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.”Methali 15:28.

BIBLIA INASEMA NINI?

Kutafakari kunakofaa huboresha utu wetu, hutuletea utulivu, na kuimarisha maadili yetu—na hivyo kufanya tuseme na kutenda kwa ufahamu na uelewaji. (Methali 16:23) Pia, kutafakari kwa njia hiyo humfanya mtu aishi maisha yenye kusudi na furaha. Kuhusu mtu anayetafakari kwa ukawaida kumhusu Mungu, andiko la Zaburi 1:3 linasema hivi: “Atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.”

Kutafakari hutusaidia pia kuboresha uwezo wetu wa kuelewa na kukumbuka mambo. Kwa mfano, tunaposoma jambo linalohusu uumbaji au habari fulani katika Biblia, tunajifunza mambo mengi mazuri. Lakini tunapotafakari mambo hayo, tunaona jinsi yanavyohusiana yenyewe na pia yanavyohusiana na yale tuliyojifunza zamani. Hivyo, kama fundi anavyotumia mbao kujenga nyumba maridadi, kutafakari hutusaidia “kukusanya” habari na kutokeza muundo wenye upatano.

Je, kutafakari kunahitaji kudhibitiwa?

“Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?”—Yeremia 17:9.

BIBLIA INASEMA NINI?

“Kutoka ndani, kutoka katika moyo wa watu, hutoka mawazo mabaya: uasherati, wizi, mauaji, uzinzi, kutamani, matendo ya uovu, udanganyifu, mwenendo mpotovu, jicho lenye wivu, . . . [na] ukosefu wa akili.” (Marko 7:21, 22) Ni lazima tudhibiti jinsi tunavyotafakari sawa tu na moto unavyodhibitiwa! La sivyo, mawazo yasiyofaa yanaweza kuchochea tamaa mbaya ambazo zinaweza kuongoza kwenye matendo maovu.—Yakobo 1:14, 15.

Kwa hiyo, Biblia inatutia moyo tutafakari ‘mambo yaliyo ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, ya kupendeka, yanayosemwa vema, yaliyo ya wema wa adili, na yanayostahili sifa.’ (Wafilipi 4:8, 9) Tukisitawisha akilini mawazo hayo yanayofaa, tutakuwa na sifa nzuri, maneno yenye neema, na mahusiano mazuri pamoja na wengine.—Wakolosai 4:6.