Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waonyeshe Huruma “Watu wa Namna Zote”

Waonyeshe Huruma “Watu wa Namna Zote”

YESU alipowafundisha wanafunzi wake jinsi ya kuhubiri habari njema, alitambua kwamba si nyakati zote watu wangekubali ujumbe huo. (Luka 10:3, 5, 6) Katika huduma yetu, huenda tukakutana na watu wakali au wakatili. Ni wazi kwamba tunapokutana na watu wa namna hiyo, inaweza kuwa vigumu kuendelea kuwaonyesha huruma watu tunaowahubiria.

Mtu mwenye huruma hutambua mahitaji na matatizo ya watu wengine, huwasikitikia, na kutamani sana kuwasaidia. Hata hivyo, tukiacha kuwahurumia watu tunaokutana nao katika huduma yetu, bidii yetu itafifia na tutashindwa kuwasaidia. Kwa upande mwingine, tunapowaonyesha wengine huruma, ni kama kuongeza kuni kwenye moto—bidii yetu katika kazi ya kuhubiri itaendelea kuwaka kwa uangavu!—1 The. 5:19.

Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwaonyesha wengine huruma hata wakati ambapo si rahisi kufanya hivyo? Acheni tuchunguze mifano mitatu inayostahili kuigwa, yaani, mfano wa Yehova, Yesu, na mtume Paulo.

IGA HURUMA YA YEHOVA

Kwa maelfu ya miaka, Yehova amevumilia kuona jina lake likichafuliwa. Licha ya hilo, yeye huendelea “[kuwaonyesha] fadhili hata watu wasio na shukrani na waovu.” (Luka 6:35) Fadhili yake huonyesha jinsi alivyo mwenye subira. Yehova anatamani “watu wa namna zote” waokolewe. (1 Tim. 2:3, 4) Ingawa Mungu anachukia uovu, yeye huwaona wanadamu wote kuwa wenye thamani na hataki yeyote aangamie.—2 Pet. 3:9.

Yehova anaelewa jinsi ambavyo Shetani amefaulu kwa kiwango kikubwa kuwapofusha wanadamu wasioamini. (2 Kor. 4:3, 4) Watu wengi wamefundishwa mafundisho ya uwongo tangu walipokuwa watoto wadogo, jambo linalofanya iwe vigumu kwao kukubali kweli. Yehova anatamani sana kuwasaidia watu wa namna hiyo. Tunajuaje?

Fikiria jinsi Yehova alivyowaona wakaaji wa jiji la kale la Ninawi. Licha ya njia zao zenye ukatili, Yehova alimwambia hivi Yona: “Je, mimi pia sipaswi kulihurumia jiji kubwa la Ninawi, ambalo lina watu zaidi ya 120,000 ambao hata hawajui kutofautisha jema na baya?” (Yona 4:11) Yehova alifahamu kwamba Waninawi hawakuwa wamepata fursa ya kumjua Yeye, naye akachochewa na rehema kumtuma Yona ili awaonye.

Kama Yehova, sisi pia tunawaona watu kuwa wenye thamani. Tunaweza kumwiga kwa kujitahidi kuwasaidia wale wote ambao wanakubali kutusikiliza, hata ingawa huenda wasikubali kweli.

IGA HURUMA YA YESU

Kama Baba yake, Yesu aliwasikitikia watu waliokuwa na uhitaji wa kiroho. “Alipoona umati akausikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Yesu alifahamu kwa undani hali yao; alitambua kwamba watu waliokuja kumsikiliza walikuwa wamefundishwa uwongo na kukandamizwa na viongozi wao wa kidini. Ingawa alijua kwamba wengi wao wangeruhusu mambo mbalimbali yawazuie kukubali ujumbe wake, bado aliendelea “kuwafundisha mambo mengi.”—Marko 4:1-9.

Usikasirike ikiwa mwanzoni mtu anakataa kusikiliza

Hali za watu za maisha hubadilika, ndivyo pia mitazamo ya watu kuelekea kweli

Watu wanapokataa ujumbe wetu, tunahitaji kuona mambo kwa undani zaidi na kujiuliza kwa nini wanaitikia kwa njia hiyo. Baadhi ya watu wana maoni yasiyofaa kuhusu Biblia au Ukristo kwa sababu wamejionea mwenendo usiofaa wa wale wanaodai kuwa Wakristo. Huenda wengine wameambiwa habari za uwongo kuhusu imani yetu. Na huenda wengine wanaogopa kudhihakiwa na watu katika jamii au watu wao wa familia ikiwa watakubali kutusikiliza.

Baadhi ya watu tunaokutana nao katika huduma wanakataa ujumbe wetu kwa sababu ya mambo mabaya waliyopitia maishani ambayo yamewaathiri kihisia. Dada mmoja mmishonari anayeitwa Kim anasema hivi: “Katika mojawapo ya maeneo tunayohubiri, watu wengi wameathiriwa na vita ambavyo vimefanya wapoteze mali zao zote. Hawana tumaini hakika la wakati ujao. Wamekata tamaa na hawamwamini yeyote. Tunapohubiri katika eneo hilo, kwa kawaida tunakutana na watu wanaopinga ujumbe wetu. Pindi moja nilishambuliwa nilipokuwa nikihubiri.”

Ni nini kinachomsaidia Kim kuendelea kuonyesha huruma licha ya kutendewa kwa njia hiyo? Anasema hivi: “Ninapotendewa kwa njia isiyofaa, ninajitahidi kukumbuka andiko la Methali 19:11 ambalo linasema: ‘Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake.’ Ninapofikiria kuhusu hali ambazo watu ninaowahubiria walipitia ninachochewa kuwaonyesha huruma. Na si kila mtu tunayekutana naye ni mkali. Katika eneo hilohilo, tumepata watu wanaotusikiliza ambao tunawarudia.”

Ni vizuri kujiuliza, ‘Ikiwa mimi ningekuwa mwenye nyumba, ningeitikiaje ujumbe wa Ufalme?’ Kwa mfano, ungeitikiaje ikiwa ungekuwa umeambiwa habari nyingi za uwongo kuhusu Mashahidi wa Yehova? Huenda wewe pia ungekataa ujumbe wa Ufalme na ungehitaji kuonyeshwa huruma. Tunapokumbuka amri ya Yesu ya kuwatendea wengine kama ambavyo tungependa kutendewa, tunachochewa kuwaonyesha wengine huruma hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo.—Mt. 7:12.

IGA HURUMA YA PAULO

Mtume Paulo aliwaonyesha huruma hata watu waliompinga vikali. Kwa nini? Kwa sababu alikumbuka jinsi alivyokuwa zamani. Alisema hivi: “Zamani nilikuwa mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau. Hata hivyo, nilionyeshwa rehema, kwa sababu nilitenda bila ujuzi na sikuwa na imani.” (1 Tim. 1:13) Alitambua kwamba Yehova na Yesu walikuwa wamemwonyesha rehema nyingi sana. Na huenda baadhi ya watu aliowahubiria walimkumbusha jinsi alivyokuwa zamani.

Nyakati nyingine Paulo alikutana na watu waliokuwa wameathiriwa sana na mafundisho ya uwongo. Alitendaje? Andiko la Matendo 17:16 linatuambia kwamba Paulo alipokuwa Athene, “roho yake ikaudhika sana alipoona kwamba jiji hilo lilikuwa limejaa sanamu.” Ingawa hivyo, Paulo alitumia jambo hilohilo lililokuwa limemuudhi kutoa ushahidi mzuri. (Mdo. 17:22, 23) Alibadili njia yake ya kuhubiri ili ipatane na hali mbalimbali za watu aliowahubiria “ili kwa vyovyote [awaokoe] wengine.”—1 Kor. 9:20-23.

Tunaweza kumwiga Paulo kwa kutambua maoni au mafundisho yasiyofaa ya watu tunaowahubiria na kisha kutumia ustadi kuwaeleza “habari njema za jambo bora.” (Isa. 52:7) Dada mmoja anayeitwa Dorothy anasema hivi: “Katika eneo letu, watu wengi wamefundishwa kuwa Mungu ni mkali na anapenda kuwahukumu tu watu. Mimi huwapongeza watu hao kwa sababu ya imani yao yenye nguvu kumwelekea Mungu na kisha ninawaonyesha kile ambacho Biblia inasema kuhusu utu wenye upendo wa Yehova na ahadi zake za wakati ujao.”

“ENDELEA KUUSHINDA UOVU KWA WEMA”

“Siku za mwisho” zinapozidi kukaribia mwisho wake, tunatarajia kwamba mitazamo ya baadhi ya watu tunaowahubiria “[itaendelea] kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.” (2 Tim. 3:1, 13) Lakini hatupaswi kuruhusu kamwe hali hiyo itufanye tuache kuwaonyesha wengine huruma, au tupoteze shangwe yetu. Yehova anaweza kutupatia nguvu za “[kuendelea] kuushinda uovu kwa wema.” (Rom. 12:21) Dada mmoja painia anayeitwa Jessica anaeleza hivi: “Mara kwa mara mimi hukutana na watu ambao si wanyenyekevu, wanaotudhalilisha, na kudharau ujumbe wetu. Hilo linaweza kumfanya mtu akasirike. Ninapoanza mazungumzo pamoja na mtu, mimi husali kwa Yehova kimyakimya nikimwomba anisaidie kumwona mtu huyo kama Yehova anavyomwona. Hilo hunifanya niache kukazia fikira hisia zangu na badala yake nifikirie jinsi ninavyoweza kumsaidia mtu huyo.”

Tunaendelea kuwatafuta watu walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele

Baadhi ya watu hukubali kutusikiliza tukiendelea kuhubiri bila kukata tamaa

Tunapaswa pia kufikiria jinsi ya kuwatia moyo wahubiri wenzetu. Jessica anasema hivi: “Mhubiri mwenzangu anapopata matokeo mabaya katika utumishi, mimi hujitahidi nisikazie fikira jambo hilo. Badala yake mimi hubadili mazungumzo na kuanza kuzungumzia mambo mazuri, kama vile mambo ambayo huduma yetu hutimiza licha ya kwamba baadhi ya watu wanakataa ujumbe wetu.”

Yehova anajua vizuri changamoto tunazokabili katika huduma. Hapana shaka anafurahi sana tunapoiga rehema yake! (Luka 6:36) Bila shaka Yehova hataendelea kuwaonyesha watu huruma yake sikuzote. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba anajua wakati hususa wa kuukomesha mfumo huu wa mambo. Hivyo kabla ya wakati huo, tunahitaji kuhubiri tukiwa na hisi ya uharaka. (2 Tim. 4:2) Acheni tuendelee kutimiza kazi yetu kwa bidii na kuwaonyesha huruma nyororo “watu wa namna zote.”