Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Wakristo wataacha kupata mwito wa tumaini la kimbingu wakati gani?

Biblia haitoi jibu kamili kwa swali hilo. Tunajua kwamba kutiwa mafuta kwa wanafunzi wa Yesu ili wapate urithi wa kimbingu kulianza mwaka wa 33 W.K. (Matendo 2:1-4) Tunajua pia kwamba baada ya kifo cha mitume, “ngano,” yaani, Wakristo wa kweli waliotiwa mafuta, na “magugu,” yaani, Wakristo wa uwongo, ‘walikua pamoja.’ (Mathayo 13:24-30) Kisha, kuanzia mwisho wa miaka ya 1800, Wakristo watiwa-mafuta walianza tena kutenda kwa bidii. Katika mwaka wa 1919 kuvuna “mavuno ya dunia,” kutia ndani kukusanywa kwa watiwa-mafuta wa mwisho, kulianza.—Ufunuo 14:15, 16.

Tangu mwishoni mwa miaka ya 1800 hadi 1931, kusudi kubwa la kazi ya kuhubiri lilikuwa kukusanya washiriki waliobaki wa mwili wa Kristo. Mnamo 1931, Wanafunzi wa Biblia walichukua jina linalotegemea Biblia, yaani, Mashahidi wa Yehova, na katika toleo la Kiingereza la Novemba 15, 1933 (15/11/1933), la Mnara wa Mlinzi, ilielezwa kwamba jina hilo la pekee ndiyo “dinari” inayotajwa katika mfano wa Yesu ulio katika Mathayo 20:1-16. Ilifikiriwa kuwa saa 12 zinazotajwa katika mfano huo zinalingana na miaka 12 kuanzia 1919 mpaka 1931. Kwa miaka mingi iliyofuata iliaminiwa kuwa mwito wa kuingia katika Ufalme wa mbinguni ulikoma katika 1931, na kwamba wale walioitwa kati ya 1930 na 1931 ili wawe warithi-washirika pamoja na Kristo walikuwa “wa mwisho” kuitwa. (Mathayo 20:6-8) Hata hivyo, katika mwaka wa 1966 uelewaji uliorekebishwa kuhusu mfano huo ulitolewa, na ikawa wazi kwamba mfano huo hauhusiani kwa vyovyote na mwisho wa kuitwa kwa watiwa-mafuta.

Mnamo 1935, ilieleweka kwamba “umati mkubwa” wa Ufunuo 7:9-15 unafanyizwa na “kondoo wengine,” Wakristo walio na tumaini la kidunia ambao wangekusanywa katika “siku za mwisho” na ambao wakiwa kikundi kimoja, wangeokoka Har–Magedoni. (Yohana 10:16; 2 Timotheo 3:1; Ufunuo 21:3, 4) Baada ya mwaka huo, kazi ya kufanya wanafunzi ilihusu hasa kukusanywa kwa umati mkubwa. Hivyo, hasa baada ya mwaka wa 1966 iliaminiwa kwamba mwito wa kimbingu ulikoma mwaka wa 1935. Ilielekea kwamba jambo hilo limethibitishwa kwa kuwa karibu watu wote waliobatizwa baada ya 1935 walihisi kwamba wana tumaini la kidunia. Tangu wakati huo, iliaminiwa kwamba wale wote waliopokea mwito wa kimbingu baada ya hapo walikuwa wakichukua mahali pa Wakristo watiwa-mafuta ambao walikosa kuwa waaminifu.

Hapana shaka kwamba, mmoja wa watiwa-mafuta akiacha kweli na akose kutubu, Yehova atamwita mtu mwingine achukue mahali pake. (Waroma 11:17-22) Hata hivyo, inaelekea kwamba idadi ya watiwa-mafuta wa kweli ambao wamekosa kuwa waaminifu si kubwa. Kwa upande mwingine, kadiri ambavyo wakati umepita, Wakristo fulani waliobatizwa baada ya mwaka wa 1935 wameshuhudiwa na roho takatifu kwamba wana tumaini la kimbingu. (Waroma 8:16, 17) Hivyo, inaonekana kwamba hatuwezi kuweka tarehe kamili ambayo Wakristo wanaacha kupokea mwito wa kimbingu.

Tunapaswa kuwa na maoni gani kumhusu mtu ambaye ameamua moyoni mwake kwamba sasa yeye ni mtiwa-mafuta na anaanza kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho? Hapaswi kuhukumiwa. Jambo hilo linamhusu yeye na Yehova. (Waroma 14:12) Hata hivyo, Wakristo ambao kwa kweli wametiwa mafuta hawadai wengine wawaone kuwa watu wa pekee. Hawaamini kwamba kuwa watiwa-mafuta kunawapa “ufahamu” wa pekee, unaozidi ule ambao washiriki fulani wenye uzoefu wa umati mkubwa wanaweza kuwa nao. Hawaamini kwamba kwa sababu ya kutiwa mafuta wana kiasi kikubwa cha roho takatifu kuliko waandamani wao wa kondoo wengine, wala hawatazamii watendewe kwa njia ya pekee au hawadai kwamba kwa sababu wanakula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho wako juu ya wazee waliowekwa rasmi kutanikoni. Wanakumbuka kwa unyenyekevu kwamba wanaume fulani waliotiwa mafuta katika karne ya kwanza hawakustahili kutumika wakiwa wazee au watumishi wa huduma. (1 Timotheo 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9; Yakobo 3:1) Wakristo fulani watiwa-mafuta hata walikuwa dhaifu kiroho. (1 Wathesalonike 5:14) Na ingawa akina dada walikuwa watiwa-mafuta, hawakufundisha kutanikoni.—1 Timotheo 2:11, 12.

Kwa hiyo, Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao kondoo wengine wanajitahidi kudumu wakiwa na nguvu kiroho, wakisitawisha tunda la roho, na wakidumisha amani katika kutaniko. Wakristo wote, iwe ni watiwa-mafuta au kondoo wengine, wanajitahidi sana kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi chini ya mwongozo wa Baraza Linaloongoza. Wakristo watiwa-mafuta wanaridhika kufanya hivyo kwa muda wote maadamu ni mapenzi ya Mungu waendelee kuwa duniani wakiwa watumishi wa Yehova.