Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtolea Yehova Dhabihu kwa Nafsi Yote

Kumtolea Yehova Dhabihu kwa Nafsi Yote

“Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova.”​—KOL. 3:23.

1-3. (a) Je, kifo cha Yesu juu ya mti wa mateso kilimaanisha kwamba Yehova hakuhitaji tena tutoe dhabihu ya aina yoyote? Eleza. (b) Ni swali gani linalozuka kuhusu dhabihu leo?

KATIKA karne ya kwanza W.K., Yehova aliwafunulia watu wake kwamba dhabihu ya fidia ya Yesu ilikuwa imefutilia mbali Sheria ya Musa. (Kol. 2:13, 14) Matoleo yote ya dhabihu ambayo Wayahudi walikuwa wakitoa kwa mamia ya miaka hayakuhitajiwa tena na hayakuwa tena na thamani yoyote. Sheria ilikuwa imetimiza kusudi lake ikiwa ‘mtunzaji wa kuongoza kwa Kristo.’​—Gal. 3:24.

2 Hilo halimaanishi kwamba Wakristo hawapendezwi tena na dhabihu. Kinyume chake, mtume Petro alizungumza kuhusu uhitaji wa “kutoa dhabihu za kiroho zenye kukubalika kwa Mungu kupitia Yesu Kristo.” (1 Pet. 2:5) Isitoshe, mtume Paulo alisema wazi kwamba maisha ya Mkristo aliyejiweka wakfu, yaani, kila sehemu ya maisha yake inaweza kwa kufaa kuonwa kuwa “dhabihu.”​—Rom. 12:1.

3 Hivyo basi, Mkristo anamtolea Yehova dhabihu kwa kumpa vitu fulani au kwa kujinyima vitu fulani kwa ajili yake. Kwa msingi wa mambo tunayojua kuhusu matakwa ambayo Waisraeli walipaswa kutimiza, tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba Yehova anakubali dhabihu zetu zote leo?

KATIKA MAISHA YA KILA SIKU

4. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu shughuli za kila siku za maisha?

4 Tunapoendelea na maisha yetu ya kila siku, huenda ikaonekana kuwa vigumu kuona uhusiano uliopo kati ya utendaji wetu na kumtolea Yehova dhabihu. Huenda kazi ya nyumbani, kazi ya shuleni, kazi ya kimwili, ununuzi, na shughuli nyingine kama hizo zikaonekana kijuu-juu kuwa hazina uhusiano mkubwa na mambo ya kiroho. Hata hivyo, ikiwa umeweka maisha yako wakfu kwa Yehova au unatumaini kufanya hivyo hivi karibuni, basi mtazamo ambao unaonyesha unaposhiriki katika utendaji huo mdogo ni muhimu. Sisi ni Wakristo kila siku muda wa saa 24. Tunapaswa kutumia kanuni za Kimaandiko katika kila sehemu ya maisha yetu. Hivyo, Paulo alituhimiza hivi: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kama kwa wanadamu.”​—Soma Wakolosai 3:18-24.

5, 6. Tunapaswa kufikiria nini kuhusu jinsi tunavyovaa na kujipamba kila siku?

5 Shughuli za Mkristo za kila siku si sehemu ya utumishi wake mtakatifu. Hata hivyo, uhakika wa kwamba Paulo anatuhimiza tufanye mambo kwa “nafsi yote kama kwa Yehova” unatufanya tufikirie maisha yetu yote. Basi tunaweza kutumiaje habari hiyo maishani mwetu? Je, tunatenda na kuvaa kwa njia inayofaa nyakati zote? Au tunaposhiriki katika utendaji mwingine wa kawaida, huenda tukaaibika kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova, labda kwa sababu ya jinsi tunavyojiendesha au jinsi tunavyovaa? Isiwe hivyo kamwe! Watu wa Yehova hawangetaka kufanya jambo lolote ambalo linaweza kuharibu sifa ya jina la Mungu.​—Isa. 43:10; 2 Kor. 6:3, 4, 9.

6 Acheni tuchunguze jinsi tamaa ya kufanya mambo “kwa nafsi yote kama kwa Yehova” inavyokuwa na uvutano katika sehemu mbalimbali za maisha. Tunapofanya hivyo, kumbuka kwamba dhabihu zote ambazo Waisraeli walimtolea Yehova zilipaswa kuwa dhabihu bora zaidi walizokuwa nazo.​—Kut. 23:19.

JINSI MAISHA YAKO YANAVYOHUSIKA

7. Ni nini kinachohusika katika wakfu wa Kikristo?

7 Ulipojiweka wakfu mwenyewe kwa Yehova, ulifanya uamuzi huo bila kusita, sivyo? Hivyo, ulisema kwamba utamtanguliza Yehova katika kila jambo maishani mwako. (Soma Waebrania 10:7.) Huo ulikuwa uamuzi mzuri. Bila shaka umeona kwamba unapofuata maoni ya Yehova kuhusu jambo fulani na kujitahidi kutenda kupatana nayo, matokeo yanakuwa bora kabisa. (Isa. 48:17, 18) Watu wa Mungu ni watakatifu na wana shangwe kwa sababu wanadhihirisha sifa za Yule anayewafundisha.​—Law. 11:44; 1 Tim. 1:11.

8. Tunajifunza nini kutokana na uhakika wa kwamba Yehova aliona dhabihu za zamani kuwa takatifu?

8 Dhabihu ambazo Waisraeli walimtolea Yehova zilionwa kuwa takatifu. (Law. 6:25; 7:1) Neno la Kiebrania ambalo limetafsiriwa kuwa “utakatifu” linatoa wazo la kujitenga, kuwa wa pekee, au kutakaswa ili kuwa mali ya Mungu. Ili Yehova akubali dhabihu zetu, ni lazima tuwe tofauti na kutochafuliwa na uvutano wa ulimwengu. Hatuwezi kupenda kitu chochote ambacho Yehova anachukia. (Soma 1 Yohana 2:15-17.) Ni wazi kwamba hilo linamaanisha ni lazima tuepuke mashirika yoyote au shughuli zozote ambazo zitatufanya tuwe wachafu machoni pa Mungu. (Isa. 2:4; Ufu. 18:4) Inamaanisha pia kwamba hatuwezi kuruhusu macho yetu yaendelee kutazama mambo yaliyo machafu au mapotovu kiadili au kuruhusu akili zetu ziwazie mambo hayo.​—Kol. 3:5, 6.

9. Mwenendo wa Mkristo kuelekea wengine ni muhimu kadiri gani, na kwa nini?

9 Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” (Ebr. 13:16) Kwa hiyo, kuwa mwema na kuwatendea wengine mema bila shaka ni jambo ambalo Yehova anaona kuwa dhabihu inayokubalika kwake. Kuwajali wengine kwa upendo ni alama inayowatofautisha Wakristo wa kweli.​—Yoh. 13:34, 35; Kol. 1:10.

DHABIHU KATIKA IBADA

10, 11. Yehova anaonaje ibada na huduma yetu ya Kikristo, na hilo linapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?

10 Njia moja iliyo wazi zaidi ambayo tukiwa Wakristo tunawatendea wengine mema ni kupitia “tangazo la hadharani la tumaini letu.” Je, unatumia kila nafasi unayopata kutoa ushahidi? Paulo aliuita utendaji huo muhimu wa Kikristo “dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina [la Mungu] tangazo la hadharani.” (Ebr. 10:23; 13:15; Hos. 14:2) Tunaweza kusema mengi kuhusu kiasi cha wakati tunachotumia katika kuhubiri habari njema ya Ufalme na jinsi tunavyoweza kuboresha njia zetu za kuhubiri, na sehemu nyingi za Mkutano wa Utumishi zimekusudiwa kutuchochea kufikiria jambo hilo. Hata hivyo, kwa ufupi, kwa kuwa utumishi wa shambani na mahubiri yasiyo rasmi ni “dhabihu ya sifa,” sehemu ya ibada yetu, basi dhabihu hiyo inapaswa kuwa dhabihu bora zaidi tunayoweza kutoa. Hali zetu zinatofautiana, ingawa hivyo, kwa kawaida kiasi cha wakati tunachotumia katika kutangaza habari njema kinaonyesha jinsi tunavyothamini mambo ya kiroho.

11 Wakristo wanatumia kwa kawaida wakati wao ili kuabudu faraghani au wakiwa kikundi. Yehova anataka tufanye hivyo. Ni kweli kwamba hatuko tena chini ya sheria kali ya kuwa na pumziko la Sabato au kufunga safari za kwenda kuhudhuria kwa ukawaida sherehe huko Yerusalemu. Hata hivyo, sherehe hizo za kale zinahusiana na mambo fulani katika maisha ya Mkristo. Bado Mungu anatutazamia tuache matendo yaliyokufa ili tujifunze Neno lake, tusali, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Na vichwa vya familia za Kikristo wanachukua hatua ili kuongoza ibada ya familia katika familia zao. (1 The. 5:17; Ebr. 10:24, 25) Kuhusu utendaji wetu wa Kikristo, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninaweza kuboresha ibada yangu?’

12. (a) Kutoa uvumba katika ibada zamani kunaweza kulinganishwa na nini leo? (b) Ulinganifu huo unapaswa kutuchochea kutoa sala za aina gani?

12 Mfalme Daudi alimwimbia Yehova hivi: “Sala yangu na itayarishwe kama uvumba mbele zako.” (Zab. 141:2) Tua kidogo na ufikirie kuhusu sala zako, kuhusu ubora na ukawaida wa sala zako. Kitabu cha Ufunuo kinalinganisha “sala za watakatifu” na uvumba kwa kuwa sala zinazokubalika zinapanda kwa Yehova kama uvumba wenye harufu nzuri na wenye kuvutia. (Ufu. 5:8) Katika Israeli la kale, uvumba ambao ulitolewa kwa kawaida juu ya madhabahu ya Yehova ulihitaji kutayarishwa kwa uangalifu na kwa njia inayofaa kabisa. Yehova alikubali uvumba huo ikiwa tu ulitolewa kulingana na maagizo ambayo alikuwa ameweka. (Kut. 30:34-37; Law. 10:1, 2) Ikiwa sala zetu za kutoka moyoni zinatayarishwa vivyo hivyo, basi tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anazikubali.

KUTOA NA KUPOKEA

13, 14. (a) Epafrodito na kutaniko la Filipi walimhudumia Paulo jinsi gani, na mtume huyo alihisije kuhusu hilo? (b) Tunaweza kuigaje mfano wa Epafrodito na Wafilipi?

13 Michango ya kifedha inayotolewa ili kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote inaweza kulinganishwa na dhabihu, iwe tunatoa mchango mkubwa au mdogo. (Marko 12:41-44) Katika karne ya kwanza W.K., kutaniko la huko Filipi lilimtuma Epafrodito aende Roma ili ashughulikie mahitaji ya kimwili ya Paulo. Ni wazi kwamba mjumbe huyo wa Wafilipi alibeba zawadi ya fedha iliyotolewa na kutaniko hilo. Hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa Wafilipi kumwonyesha Paulo ukarimu. Walimtendea Paulo kwa fadhili kwa sababu hawakutaka awe na mahangaiko ya kifedha, badala yake, walitaka atumie wakati zaidi katika huduma. Paulo alionaje zawadi hiyo? Aliita zawadi hiyo “harufu tamu, dhabihu yenye kukubalika, inayompendeza Mungu vyema.” (Soma Wafilipi 4:15-19.) Kwa kweli Paulo alithamini tendo hilo lenye fadhili la Wafilipi, na Yehova pia alilithamini.

14 Vivyo hivyo leo, Yehova anathamini sana michango tunayotoa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Zaidi ya hayo, anaahidi kwamba tukiendelea kutanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yetu, atatosheleza mahitaji yetu yote, ya kiroho na ya kimwili.​—Mt. 6:33; Luka 6:38.

ONYESHA UTHAMINI WAKO

15. Ni baadhi ya mambo gani yanayokufanya umshukuru Yehova?

15 Tuna sababu nyingi sana za kumshukuru Yehova. Je, si kweli kwamba kila siku tunapaswa kumshukuru kwa sababu ya zawadi ya uhai? Anatupatia kila kitu tunachohitaji ili kuendeleza uhai wetu, yaani, chakula, mavazi, na makao na pia hewa tunayopumua. Isitoshe, imani yetu, inayotegemea ujuzi inatupatia tumaini. Inafaa kwetu kumwabudu Yehova na kutoa dhabihu za sifa za kumsifu, hasa kwa sababu ya sifa zake na yale ambayo ametufanyia.​—Soma Ufunuo 4:11.

16. Tunapaswa kutendaje kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Kristo?

16 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, zawadi yenye thamani sana ambayo Mungu amewapa wanadamu ni dhabihu ya fidia ya Kristo. Mungu ametuonyesha upendo wa pekee kwa kutoa dhabihu hiyo. (1 Yoh. 4:10) Ni njia gani inayofaa ya kumshukuru Mungu kwa sababu ya zawadi hiyo? Paulo alitangaza hivi: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote; . . . naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.” (2 Kor. 5:14, 15) Kwa kweli, kile ambacho Paulo alikuwa akisema ni kwamba ikiwa tunathamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu tutatumia maisha yetu kumheshimu Mungu na Mwana Wake. Tunaonyesha kwamba tunampenda na kumthamini Mungu na Kristo kwa kutii na kwa tamaa yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi.​—1 Tim. 2:3, 4; 1 Yoh. 5:3.

17, 18. Ni katika njia zipi wengine wameongeza dhabihu yao ya sifa kwa Yehova? Toa mfano.

17 Je, unaweza kuboresha dhabihu ya sifa unayomtolea Mungu? Baada ya kutafakari mambo yote mema ambayo Yehova amewafanyia, wengi wamechochewa kuratibu wakati wao na utendaji wao ili kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme au katika utendaji mwingine wa kitheokrasi. Wengine wamekuwa wakifanya upainia msaidizi kwa mwezi mmoja au zaidi kila mwaka, na wengine wamekuwa mapainia wa kawaida. Na kuna wengine ambao wameshiriki katika miradi ya ujenzi wa majengo yanayotumiwa kwa kazi ya Ufalme. Je, hizo si njia bora sana za kuonyesha uthamini wetu? Mungu anakubali matendo hayo ya utumishi mtakatifu ikiwa yanafanywa kwa nia inayofaa, yaani, ili kuonyesha uthamini na shukrani.

18 Wakristo wengi wamehisi kwamba wana deni la kumshukuru Yehova na limewachochea kufanya hivyo. Morena ni kati ya Wakristo hao. Alitafuta majibu ya maswali yake ya kiroho katika falsafa za Asia na katika Ukatoliki, dini ya wazazi wake. Lakini hakupata majibu yenye kuridhisha. Kiu yake ya kiroho ilitoshelezwa wakati tu alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Morena alithamini sana kupata majibu yaliyo wazi ya Kimaandiko kwa maswali yake yote ambayo pia yaliimarisha maisha yake hivi kwamba alitaka kumshukuru Yehova kwa kutumia nguvu zake zote kumtumikia. Alianza kufanya upainia msaidizi kwa ukawaida baada tu ya kubatizwa, na hali zilipomruhusu akawa painia wa kawaida. Miaka 30 imepita sasa, na Morena angali katika utumishi wa wakati wote.

19. Unaweza kuongeza jinsi gani dhabihu zako za sifa kwa Yehova?

19 Bila shaka, kuna watumishi wengi waaminifu wa Yehova ambao hawawezi kutumikia wakiwa mapainia kwa sababu hali zao haziwaruhusu. Sote tunaweza kumtolea Yehova dhabihu za kiroho zinazokubalika katika jambo lolote lile tunaloweza kufanya katika utumishi wake. Katika mwenendo wetu, tunahitaji kufuata kwa makini kanuni za uadilifu, tukikumbuka kwamba tunamwakilisha Yehova nyakati zote. Kwa imani, tunakuwa na uhakika kamili kwamba makusudi ya Mungu yatafanikiwa. Kwa kazi njema, tunasaidia kueneza habari njema. Tunaonyesha kwa kweli kwamba tunamshukuru Yehova kwa yote ambayo ametufanyia kwa kuendelea kumtolea dhabihu kwa nafsi yetu yote.

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 25]

Je, wema wa Yehova unakuchochea kuboresha dhabihu yako ya sifa?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, unatumia kila nafasi unayopata kutoa ushahidi?