Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Kuwa ‘Umemjua Mungu,’ Ufanye Nini Sasa?

Kwa Kuwa ‘Umemjua Mungu,’ Ufanye Nini Sasa?

“Mmemjua Mungu.”—GAL. 4:9.

1. Kwa nini rubani anahitaji kufuata orodha ya ukaguzi kabla ya ndege kupaa angani?

MARUBANI wanaoendesha ndege bora zaidi duniani huwa na orodha yenye mambo zaidi ya 30 wanayopaswa kukagua kabla ya kuanza safari. Marubani hao wasipofuata kwa uangalifu orodha hiyo ya ukaguzi kila mara wanapotaka kupaa angani, kuna uwezekano mkubwa zaidi wa ndege kuanguka. Je, unajua ni rubani yupi hasa anayehimizwa ajaze orodha hiyo kila mara? Ni yule mwenye uzoefu mwingi zaidi! Ni rahisi sana kwa rubani mwenye uzoefu kuwa asiyejali na hivyo kutofanya ukaguzi huo kikamili kabla ya kupaa angani.

2. Wakristo wanatiwa moyo kufanya uchunguzi gani?

2 Kama rubani anayezingatia usalama, unaweza kutumia orodha kama hiyo kuhakikisha kwamba imani yako haiyumbiyumbi unapokabili matatizo. Iwe umebatizwa hivi karibuni au umekuwa ukimtumikia Mungu kwa miaka mingi, ni muhimu sana uchunguze kwa ukawaida kina cha imani yako na ujitoaji wako kwa Yehova Mungu. Usipofanya hivyo kwa ukawaida na kwa bidii, unaweza kufa kiroho. Biblia inatuonya hivi: “Yeye anayefikiri kuwa amesimama na ajihadhari kwamba asianguke.”—1 Kor. 10:12.

3. Wakristo walioishi Galatia walihitaji kufanya nini?

3 Wakristo walioishi Galatia walihitaji kuchunguza kina cha imani yao na kuthamini uhuru wao wa kiroho. Kupitia dhabihu ya Yesu, wale wanaomwamini wangeweza kumjua Mungu kwa njia ya pekee sana, yaani, kuwa wana wa Mungu! (Gal. 4:9) Ili waendelee kufurahia uhusiano huo wenye thamani sana, Wagalatia walihitaji kukataa mafundisho ya Wayudaiza waliosisitiza Sheria ya Musa ifuatwe. Watu wa Mataifa wasiotahiriwa walioshirikiana na makutaniko ambao hawakuwa kamwe chini ya Sheria wangewezaje kufanya hivyo? Wayahudi na Watu wa Mataifa walihitaji kufanya  maendeleo ya kiroho. Hilo lilitia ndani kutambua kwamba hawangeweza kuwa waadilifu kwa msingi wa Sheria ya Musa.

HATUA ZA KWANZA ZA KUMJUA MUNGU

4, 5. Paulo aliwapa Wagalatia shauri gani, na shauri hilo linatuhusuje?

4 Shauri la mtume Paulo kwa Wagalatia liliandikwa kwa kusudi hili: kuwazuia Wakristo wote wa kweli wasiache utajiri wa kweli ya Biblia na kurudia mambo waliyoacha nyuma. Yehova alimwongoza mtume huyo kwa roho takatifu ili awatie moyo waabudu Wake wote waendelee kuwa imara, na si wale tu waliokuwa katika makutaniko ya Galatia.

5 Ni vizuri sote tukumbuke jinsi tulivyowekwa huru kutoka katika utumwa wa kiroho na kuwa Mashahidi wa Yehova. Fikiria maswali haya mawili: Je, unakumbuka hatua ulizochukua ili ustahili kubatizwa? Je, unakumbuka jinsi ulivyomjua na kujulikana na Mungu na hivyo kufurahia uhuru wa kweli wa kiroho?

6. Ni orodha gani ya ukaguzi tutakayochunguza?

6 Kimsingi, sote tulifuata hatua tisa. Hatua hizo ni kama orodha ya ukaguzi wa kiroho, na zimeonyeshwa katika sanduku lenye kichwa  “Hatua Zinazoongoza Kwenye Ubatizo na Kuendelea Kukua Kiroho.” Kujikumbusha kwa ukawaida hatua hizo tisa kutatuimarisha ili tuepuke kurudia vitu tulivyoacha nyuma katika ulimwengu. Kama vile tu rubani mwenye uzoefu na aliye mwangalifu anavyochunguza kwanza orodha ya ukaguzi na hivyo kuendesha ndege kwa usalama, wewe pia utaendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu ikiwa utachunguza orodha ya ukaguzi wa kiroho.

WALE AMBAO MUNGU ANAWAJUA WANAENDELEA KUKUA KIROHO

7. Tunahitaji kufuata kielelezo gani, na kwa nini?

7 Orodha ya ukaguzi humkumbusha rubani kwamba kuna mambo ya kawaida anayopaswa kukagua kwa makini kabla ya kila safari. Sisi pia tunaweza kujichunguza kwa ukawaida na kuchunguza ratiba ambayo tumekuwa tukifuata tangu tulipobatizwa. Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Endelea kushika kielelezo cha maneno yenye afya uliyosikia kutoka kwangu pamoja na imani na upendo vinavyohusiana na Kristo Yesu.” (2 Tim. 1:13) ‘Maneno hayo yenye afya’ yako katika Neno la Mungu. (1 Tim. 6:3) Kama vile tu mchoro unavyoweza kutuonyesha kwa ujumla jinsi kitu fulani kilivyo, ‘kielelezo cha ile kweli’ hutuonyesha kwa ujumla mambo ambayo Yehova anataka tujue na kufuata. Kwa hiyo, acheni sasa tuchunguze hatua zilizotuongoza kwenye ubatizo na tuone ikiwa tunafuata kwa ukaribu kielelezo cha ile kweli.

8, 9. (a) Kwa nini tunapaswa kuendelea kukua katika imani na ujuzi? (b) Toa mfano unaoonyesha umuhimu wa kukua kiroho na kwa nini tunapaswa kuendelea kukua kiroho.

8 Jambo la kwanza katika orodha yetu ya ukaguzi ni uhitaji wa kupata ujuzi. Kisha, tunaweza kusitawisha imani. Hata hivyo, tunapaswa kuendelea kukua katika ujuzi na imani. (2 The. 1:3) Kukua hutia ndani kuendelea kubadilika hatua kwa hatua. “Kukua” ni kuongezeka, kupanuka. Kwa hiyo, baada ya kubatizwa, tunahitaji kuendelea kusitawisha hali yetu ya kiroho ili tusibaki palepale kiroho.

Mti huendelea kukua ndivyo na Wakristo wanavyopaswa pia kuendelea kukua

9 Tunaweza kulinganisha ukuzi wetu wa kiroho na ukuzi wa mti. Mti unaweza kusitawi na kuwa mkubwa sana, hasa ikiwa mizizi yake imepenya ndani sana ya udongo au imeenea sana. Kwa mfano, mierezi fulani mikubwa ya Lebanoni inaweza kufikia urefu wa jengo lenye ghorofa 12, kuwa na mizizi inayopenya ndani sana ya udongo na shina lenye ukubwa wa karibu mita 12. (Wim. 5:15) Mwanzoni mwerezi hukua haraka, kisha huendelea kukua polepole bila watu kutambua. Kila mwaka, shina hupanuka,  mizizi hupenya chini zaidi na kuenea, na mti huo unakuwa imara zaidi. Hivyo ndivyo ukuzi wa kiroho wa Mkristo ulivyo. Tunapoanza kujifunza Biblia, huenda tukakua haraka kiroho na kisha kubatizwa. Washiriki wa kutaniko hufurahia maendeleo tunayofanya. Huenda hata tukastahili kuwa mapainia au tukapata mapendeleo mengine. Miaka inayofuata, huenda ukuzi wetu wa kiroho usionekane wazi kama mwanzoni. Hata hivyo, bado tunapaswa kuendelea kukua katika imani na ujuzi “kufikia kuwa mtu aliyekomaa, kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo.” (Efe. 4:13) Kwa hiyo, tunapofanya maendeleo na kuwa Wakristo wakomavu, tunakuwa kama mche mdogo unaositawi na kuwa mti mkubwa sana.

10. Kwa nini Wakristo wakomavu wanapaswa pia kuendelea kukua kiroho?

10 Lakini ukuzi wetu haupaswi kuishia hapo. Ujuzi wetu unapaswa kuongezeka na imani yetu inapaswa kutia mizizi. Hivyo, tunakuwa imara zaidi katika udongo wa Neno la Mungu. (Met. 12:3) Katika kutaniko la Kikristo, kuna ndugu na dada wengi ambao wamefanya hivyo. Kwa mfano, ndugu mmoja ambaye amekuwa mzee wa kutaniko kwa miaka zaidi ya thelathini alisema kwamba bado anaendelea kukua kiroho. Anasema hivi: “Uthamini wangu kuelekea Biblia umeongezeka sana. Kila mara, ninapata fursa mpya za kutumia kanuni na sheria za Biblia katika njia mbalimbali. Ninaendelea kuithamini zaidi huduma.”

ENDELEA KUKUA KATIKA URAFIKI WAKO PAMOJA NA MUNGU

11. Tunawezaje kumjua Yehova vizuri zaidi kadiri wakati unavyopita?

11 Ukuzi wetu unatia ndani pia kumkaribia Yehova zaidi akiwa Rafiki na Baba yetu. Anataka tuhisi kwamba tunathaminiwa. Anataka tujue kwamba tunapendwa na tuko salama kama vile mtoto anavyohisi anapendwa na yuko salama anapokumbatiwa na mzazi anayejali au kama tunavyohisi tunapokuwa na rafiki wa kweli mshikamanifu. Kama ujuavyo, urafiki wa aina hiyo pamoja na Yehova hausitawi kwa siku moja. Bila shaka, ni lazima tutumie wakati ili kumjua na kumpenda. Kwa hiyo, ili kumjua Yehova vizuri, azimia kutenga wakati wa kusoma Neno lake kila siku. Soma kila toleo la Mnara wa Mlinzi, Amkeni! na machapisho mengine yanayotegemea Biblia.

12. Ni lazima tufanye nini ili Yehova atujue?

12 Rafiki za Mungu hukua kiroho wanaposali kwa unyoofu na kushirikiana na marafiki wazuri. (Soma Malaki 3:16.)  ‘Masikio ya Yehova yanaielekea dua yao.’ (1 Pet. 3:12) Sawa na baba mpendwa, Yehova anasikiliza kwa makini vilio vyetu vya kuomba msaada. Kwa hiyo, tunahitaji ‘kudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) Bila msaada wa Mungu hatuwezi kuendelea kuwa Wakristo wakomavu. Mikazo ya mfumo huu ni mikubwa sana hivi kwamba hatuwezi kuishinda kwa uwezo wetu. Tusipoendelea kudumu katika sala, tunajitenga wenyewe na Mungu na kukosa nguvu ambazo Mungu anaweza na yuko tayari kutupatia daima. Je, umeridhika na ubora wa sala zako, au unaona kwamba kuna uhitaji wa kuziboresha?—Yer. 16:19.

13. Kwa nini ni muhimu kushirikiana na Wakristo wenzetu ili tukue kiroho?

13 Yehova anapendezwa na wale wote “wanaotafuta kimbilio kwake”; kwa hiyo, hata baada ya kumjua Mungu, tunapaswa kuendelea kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko la wengine wanaomjua. (Nah. 1:7) Katika ulimwengu uliojaa mambo yenye kuvunja moyo, ni jambo la hekima kwetu kushirikiana na ndugu na dada zetu wanaotutia moyo. Utafaidikaje? Katika kutaniko, utapata watu watakaokuchochea “katika upendo na matendo mazuri.” (Ebr. 10:24, 25) Ili kufurahia upendo wa kweli ambao Paulo alitaja katika barua yake kwa Waebrania, ni lazima tuwe sehemu ya undugu, yaani, jamii ya waabudu wenye nia moja—kutaniko. Kuonyesha upendo wa aina hiyo kunatia ndani kushirikiana na Wakristo wengine. Chunguza kwa ukawaida mazoea yako ya kuhudhuria na kutoa maelezo katika mikutano.

14. Ni kwa nini tunapaswa kuendelea kutubu na kugeuka?

14 Mwanzoni tulihitaji kutubu na kugeuka, au kuacha dhambi zetu ili tuwe Wakristo. Hata hivyo, tunapaswa kuendelea kutubu. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, dhambi inakaa ndani yetu kama nyoka aliye tayari kutushambulia. (Rom. 3:9, 10; 6:12-14) Acheni tuendelee kuwa macho na kutopuuza makosa yetu. Inatia moyo kwamba Yehova hutuonyesha subira tunapojitahidi kushinda udhaifu wetu na kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. (Flp. 2:12; 2 Pet. 3:9) Kutumia wakati na mali zetu kwa busara, na kutofuatilia mapendezi ya kichoyo kunaweza kutusaidia sana. Dada mmoja aliandika hivi: “Nililelewa katika kweli, lakini maoni yangu kumhusu Yehova yalikuwa tofauti na ya wengi. Nilihisi kwamba Yehova anapaswa kuogopwa sana, na hivyo singeweza kamwe kumpendeza.” Baadaye, dada huyo alianza “kuyumbayumba kiroho” kwa sababu ya matatizo kadhaa ya kibinafsi. Aliendelea kusema hivi: “Si kwamba sikumpenda Yehova, ukweli ni kwamba sikumjua vizuri. Hata hivyo, baada ya kusali sana kutoka moyoni, nilianza kufanya mabadiliko.” Aliongezea hivi: “Niligundua kwamba Yehova alikuwa akiniongoza kama mtoto. Akinisaidia kwa fadhili sana kushinda kizuizi kimoja baada ya kingine, na kunionyesha nilichopaswa kufanya.”

15. Yesu na Baba yake wanaona nini?

15 Semeni na watu” kuhusu habari njema. Baada ya Petro na mitume wengine kuwekwa huru kimuujiza kutoka gerezani, malaika wa Mungu aliwaambia maneno hayo. (Mdo. 5:19-21) Naam, tunapaswa pia kuchunguza jinsi tunavyoshiriki katika utumishi wa shambani kila juma. Yesu na Baba yake wanaona imani na huduma yetu. (Ufu. 2:19) Mzee aliyenukuliwa mwanzoni anasema hivi: “Jambo muhimu maishani mwetu ni huduma ya shambani.”

16. Kwa nini ni vizuri kutafakari kuhusu wakfu wetu kwa Yehova?

16 Tafakari kuhusu wakfu wako. Uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova ndicho kitu chenye thamani zaidi tulicho nacho.  Anawajua wale ambao ni mali yake. (Soma Isaya 44:5.) Sali na kuchanganua ubora na kina cha uhusiano wako pamoja naye. Kumbuka pia siku uliyobatizwa na usiisahau tarehe hiyo muhimu. Kufanya hivyo kutakukumbusha pia kwamba ulipobatizwa, ulifanya uamuzi bora zaidi maishani.

KAA KARIBU NA YEHOVA HUKU UKIVUMILIA

17. Kwa nini tunahitaji uvumilivu ili tukae karibu na Yehova?

17 Alipowaandikia Wagalatia, Paulo alikazia umuhimu wa kuonyesha uvumilivu. (Gal. 6:9) Leo pia uvumilivu ni muhimu kwa kila Mkristo. Utakabili majaribu, lakini Yehova atakusaidia. Endelea kusali ili upate roho takatifu. Utakuwa na shangwe badala ya huzuni na amani badala ya kuwa na uchungu moyoni. (Mt. 7:7-11) Fikiria hili: Ikiwa Yehova anawajali ndege, je, hakujali zaidi wewe unayempenda na uliyejitoa kumtumikia? (Mt. 10:29-31) Hata iwe unakabili matatizo gani, usirudi nyuma kamwe, usikate tamaa kamwe. Tuna utajiri mwingi kama nini kwa sababu ya kujulikana na Yehova!

18. Kwa kuwa “umemjua Mungu,” unataka kufanya nini sasa?

18 Hivyo basi, ikiwa umemjua Mungu na kubatizwa hivi karibuni, ufanye nini? Endelea kumjua Yehova vizuri zaidi na kukua kufikia ukomavu wa kiroho. Ikiwa ulibatizwa miaka mingi iliyopita, ufanye nini? Wewe pia ni lazima uendelee kutia mizizi na kuongeza ujuzi wako kumhusu Yehova. Tusitosheke kamwe na uhusiano tulio nao pamoja naye. Badala yake, sote tunapaswa kuichunguza orodha yetu ya kiroho mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kukua katika uhusiano wetu pamoja na Baba, Rafiki, na Mungu wetu Mpendwa, Yehova.—Soma 2 Wakorintho 13:5, 6.