Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Tunavyoweza Kuwasaidia Wenye Uhitaji

Jinsi Tunavyoweza Kuwasaidia Wenye Uhitaji

“MAPIGANO yalianza baada ya matokeo ya uchaguzi kutangazwa, na hivyo maelfu ya Mashahidi wa Yehova walilazimika kukimbia. Kulikuwa na upungufu wa dawa na chakula. Na vitu hivyo vilikuwa ghali mno. Benki zilifungwa na mashine za kutoa pesa hazikuwa zikifanya kazi,” akasema François, mzee wa kutaniko katika nchi moja inayoendelea.

Bila kukawia, ndugu kutoka katika ofisi ya tawi walianza kupeleka pesa na vitu vingine ili kuwasaidia Mashahidi waliokimbilia kwenye Majumba ya Ufalme kote nchini. Vikundi vilivyokuwa vikipigana viliweka vizuizi barabarani, lakini magari ya ofisi ya tawi yaliruhusiwa kupita kwa kuwa vikundi vyote vilijua kwamba Mashahidi hawaungi mkono upande wowote.

François anasema: “Tulipokuwa tukielekea kwenye Jumba moja la Ufalme, gari letu lilimiminiwa risasi. Hata hivyo, hatukujeruhiwa. Tulipomwona mwanajeshi mwenye silaha akikimbia kutuelekea, tulirudisha gari nyuma kwa kasi, tukageuka, na kurudi haraka kwenye ofisi ya tawi. Tulimshukuru Yehova kwamba tulikuwa hai. Siku iliyofuata, ndugu 130 waliokuwa katika Jumba hilo la Ufalme walikimbilia eneo lingine. Baadhi yao walikuja kwenye ofisi ya tawi, na tuliwaandalia mahitaji ya kiroho na ya kimwili hadi mapigano yalipokwisha.”

François anasema hivi: “Baadaye, ofisi ya tawi ilipokea barua nyingi kutoka kwa ndugu kote nchini wakishukuru sana kwa msaada waliopata. Uhakika wao kumwelekea Yehova uliimarika sana walipoona jinsi ndugu zao walivyowasaidia.”

Wakati wa misiba ya asili na ile inayosababishwa na wanadamu, hatuwaambii ndugu na dada zetu wenye uhitaji ‘wajipashe moto na kula vizuri.’ (Yak. 2:15, 16) Badala yake, tunajitahidi kuwaandalia mahitaji yao ya kimwili. Vivyo hivyo, baada ya Wakristo wa karne ya kwanza kuonywa kuhusu njaa kali iliyokuwa ikija, “wanafunzi wakaamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, wafanye huduma ya kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea.”—Mdo.11:28-30.

Tukiwa watumishi wa Yehova, tuko tayari kuwasaidia wenzetu walio na uhitaji wa kimwili. Hata hivyo, watu wana uhitaji wa kiroho pia. (Mt. 5:3) Ili kuwasaidia waone uhitaji huo na kuchukua hatua za kuutosheleza, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kila mmoja wetu hutumia mali, nguvu, na wakati mwingi kutimiza kazi hiyo. Tukiwa tengenezo, tunatumia kiasi fulani cha michango kuwasaidia wengine kimwili, lakini michango inayotolewa hutumiwa hasa kuendeleza kazi ya Ufalme na kueneza habari njema. Kwa njia hiyo, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na jirani.Mt. 22:37-39.

Wale wanaotegemeza kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova wana hakika kwamba michango yao inatumiwa ifaavyo. Je, unaweza kuwasaidia ndugu zako wenye uhitaji? Je, ungependa kutegemeza kazi ya kufanya wanafunzi? Ikiwa ndivyo, “usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.”Met. 3:27.