Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuzaliwa Mara ya Pili—Je, Ni Njia ya Kupata Wokovu?

Kuzaliwa Mara ya Pili—Je, Ni Njia ya Kupata Wokovu?

Kuzaliwa Mara ya Pili—Je, Ni Njia ya Kupata Wokovu?

UNGEJIBU jinsi gani swali hili: “Je, umezaliwa mara ya pili?” Mamilioni ya wanadini ulimwenguni wangejibu kwa mkazo, “Ndiyo!” Wanaamini kwamba, kuzaliwa mara ya pili, au kuzaliwa tena, kunawatambulisha Wakristo wote wa kweli na ndiyo njia pekee ya kupata wokovu. Maoni yao ni sawa na ya viongozi fulani wa dini kama mwanatheolojia Robert C. Sproul, aliyeandika hivi: “Ikiwa mtu hajazaliwa mara ya pili, . . . basi yeye si Mkristo.”

Je, wewe ni mmoja wa wale wanaoamini kwamba kuzaliwa tena ndiyo njia ya kupata wokovu? Ikiwa ndivyo, bila shaka ungependa kuwasaidia watu wa jamaa yako na marafiki waipate njia hiyo na kuanza kuifuata. Lakini ili wafanye hivyo, wanahitaji kuelewa tofauti kati ya mtu aliyezaliwa tena na yule ambaye hajazaliwa tena. Unaweza kuwaeleza jinsi gani maana ya kuzaliwa tena?

Wengi wanaamini kwamba maneno “kuzaliwa tena” yanarejelea mtu anayetoa ahadi nzito kwamba atamtumikia Mungu na Kristo, na kwa njia hiyo anaanza kuwa na uhusiano na Mungu ambao unakubalika. Kamusi moja ya karibuni inamfafanua mtu aliyezaliwa tena kuwa “Mkristo aliyeokoka.”—TUKI English-Swahili Dictionary—Toleo la Tatu.

Je, ungeshangaa kujua kwamba Biblia haisemi hivyo? Je, ungependa kujua Neno la Mungu linafundisha nini kuhusu kuzaliwa tena? Bila shaka utafaidika ukichunguza kwa makini habari kuhusu kuzaliwa tena. Kwa nini? Kwa sababu kuelewa kwa usahihi jambo hilo kunahusisha maisha yako na matarajio yako ya wakati ujao.

Biblia Inafundisha Nini?

Katika Biblia nzima, maneno “kuzaliwa tena,” au kuzaliwa mara ya pili, yanapatikana tu katika andiko la Yohana 3:1-12, linalosimulia mazungumzo yenye kupendeza kati ya Yesu na kiongozi fulani wa dini huko Yerusalemu. Simulizi hilo lote la Biblia limenukuliwa katika sanduku kwenye ukurasa wa 4. Tunakutia moyo usome habari hiyo kwa makini.

Katika simulizi hilo, Yesu anakazia mambo kadhaa kuhusu “kuzaliwa upya.” * Kwa kweli, mazungumzo ya Yesu yanatusaidia kujibu maswali haya matano muhimu:

▪ Kuzaliwa upya ni muhimu kadiri gani?

Je, mtu binafsi anaweza kuamua kuzaliwa upya?

▪ Kusudi la kuzaliwa upya ni nini?

Mtu anazaliwa upya jinsi gani?

Uhusiano kati ya Yehova na yule anayezaliwa upya unabadilika jinsi gani?

Tutachunguza maswali hayo moja baada ya lingine.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 8 Maneno “kuzaliwa upya” yanapatikana katika 1 Petro 1:3, 23. Maneno hayo ya Biblia yana maana sawa na “kuzaliwa tena,” au kuzaliwa mara ya pili, nayo yanatokana na neno la Kigiriki, gen·naʹo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

“Ninyi Lazima Mzaliwe Tena”

“Basi kulikuwa na mtu mmoja kati ya Mafarisayo, aliyeitwa Nikodemo, mtawala wa Wayahudi. Huyo alimjia wakati wa usiku na kumwambia: ‘Rabi, tunajua kwamba wewe ukiwa mwalimu umekuja kutoka kwa Mungu; kwa maana hakuna anayeweza kufanya ishara hizi ambazo unafanya isipokuwa Mungu awe pamoja naye.’ Yesu akajibu akamwambia: ‘Kwa kweli kabisa ninakuambia, Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.’ Nikodemo akamwambia: ‘Mtu anawezaje kuzaliwa akiwa mzee? Je, anaweza kuingia katika tumbo la uzazi la mama yake mara ya pili na kuzaliwa?’ Yesu akajibu: ‘Kwa kweli kabisa ninakuambia, Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu. Kile ambacho kimezaliwa kwa mwili ni mwili, na kile ambacho kimezaliwa kwa roho ni roho. Usistaajabu kwa sababu nimekuambia, Ninyi lazima mzaliwe tena. Upepo huvuma mahali ambapo unataka, nawe unasikia mvumo wake, lakini hujui mahali ambapo huo unatoka wala mahali unapoenda. Ndivyo alivyo kila mtu ambaye amezaliwa kwa roho.’ Nikodemo akajibu, akamwambia: ‘Mambo haya yanaweza kutukia jinsi gani?’ Yesu akajibu, akamwambia: ‘Je, wewe ni mwalimu wa Israeli na bado hujui mambo haya? Kwa kweli kabisa ninakuambia, Yale tunayoyajua tunayasema na yale ambayo tumeyaona tunatoa ushahidi juu yake, lakini ninyi hampokei ushahidi ambao tunatoa. Ikiwa nimewaambia ninyi mambo ya duniani na bado hamwamini, mtaamini jinsi gani nikiwaambia mambo ya mbinguni?’” —Yohana 3:1-12.