Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

1 Jifunze Kuitegemea Biblia

1 Jifunze Kuitegemea Biblia

1 Jifunze Kuitegemea Biblia

“Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.”—2 Timotheo 3:16.

KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Watu wengi wanasema kwamba Biblia ni kitabu chenye hekima ya wanadamu tu. Baadhi yao wanaamini kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu matukio katika historia si sahihi. Wengine wanadai kwamba mashauri ya Biblia hayafai na yamepitwa na wakati.

UNAWEZA KUFAULU JINSI GANI? Mara nyingi watu wasioitegemea Biblia au wale wanaofikiri kwamba haifai, hawajaichunguza. Wanasema tu mambo ambayo wamesikia wengine wakisema. Hata hivyo, Biblia inaonya: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

Badala ya kukubali bila uthibitisho mambo ambayo wengine wanasema, unaweza kufuata mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza walioishi Beroya. Jiji hilo lilikuwa katika eneo lililo kaskazini mwa Ugiriki ya sasa. Hawakukubali tu mambo waliyoambiwa na wengine. Badala yake, walikuwa na zoea la “[ku]yachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:11) Hebu tuchunguze kwa ufupi sababu mbili zinazoweza kufanya uwe na hakika kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho.

Biblia ni sahihi kihistoria. Kwa miaka mingi, watu wametilia shaka usahihi wa majina ya watu na maeneo mbalimbali ambayo Biblia inataja. Lakini, mara nyingi uthibitisho umeonyesha kuwa madai yao hayana msingi na kwamba masimulizi ya Biblia yanategemeka.

Kwa mfano, wakati fulani wasomi walisema kwamba Sargoni, Mfalme wa Ashuru anayetajwa katika Isaya 20:1, hakuwahi kuishi. Hata hivyo, katika miaka ya 1840, wataalamu wa vitu vya kale walianza kuchimbua jumba la mfalme huyo. Sasa, Sargoni ni mmojawapo wa wafalme Waashuru wanaojulikana sana.

Wachambuzi hawakuamini kwamba Pontio Pilato, gavana Mroma aliyeagiza Yesu auawe, aliwahi kuishi. (Mathayo 27:1, 22-24) Lakini mwaka wa 1961 jiwe lenye jina na cheo cha Pilato lilipatikana karibu na jiji la Kaisaria nchini Israel.

Gazeti U.S.News & World Report la Oktoba 25, 1999 (25/10/1999), linasema hivi kuhusu usahihi wa Biblia kihistoria: “Wataalamu wa vitu vya kale wa siku hizi wamethibitisha kwamba matukio muhimu katika Agano la Kale na Agano Jipya ni sahihi. Matukio hayo yanahusu mababu wa Israeli, kutoka kwa Waisraeli nchini Misri, utawala wa ukoo wa Daudi, na maisha katika siku za Yesu.” Ingawa imani katika Biblia haitegemei uvumbuzi wa vitu vya kale, ungetarajia kitabu kilichoongozwa na roho ya Mungu kiwe sahihi kihistoria.

Hekima iliyo katika Biblia inawanufaisha watu wa aina zote. Muda mrefu kabla ya kugunduliwa kwa vijidudu na jinsi vinavyoeneza magonjwa, Biblia ilikuwa imependekeza hatua fulani za kudumisha usafi ambazo bado zinafaa leo. (Mambo ya Walawi 11:32-40; Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Watu wa familia wanaofuata mashauri ya Biblia kuhusu jinsi wanavyopaswa kutendeana wanakuwa na furaha zaidi. (Waefeso 5:28–6:4) Pia, mtu anayefuata kanuni za Biblia anaweza kuwa mfanyakazi mwenye kutegemeka au mwajiri mwenye usawaziko. (Waefeso 4:28; 6:5-9) Kufuata kanuni za Biblia kunatunufaisha kihisia na kiafya vilevile. (Methali 14:30; Waefeso 4:31, 32; Wakolosai 3:8-10) Tungetarajia mashauri mazuri kama hayo kutoka kwa Muumba wetu.

UTAPATA THAWABU GANI? Hekima iliyo katika Biblia inaweza kumfanya hata mtu asiye na uzoefu awe na hekima. (Zaburi 19:7) Isitoshe, tukiitegemea Biblia, inaweza kutusaidia kuchukua hatua ya pili inayozungumziwa hapa chini ili kusitawisha imani imara. Hakuna kitabu kingine chochote kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo.

Ili kupata habari zaidi, ona sura ya 2, “Biblia—Kitabu Kutoka kwa Mungu,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 12 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.