Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Aliendelea Kukua Akiwa na Yehova’

‘Aliendelea Kukua Akiwa na Yehova’

Igeni Imani Yao

‘Aliendelea Kukua Akiwa na Yehova’

SAMWELI aliwatazama watu wake. Taifa lilikuwa limekusanyika katika mji wa Gilgali, baada ya kuitwa na mtumishi huyo mwaminifu ambaye alikuwa ametumika akiwa nabii na mwamuzi kwa muda mrefu. Ilikuwa kati ya mwezi wa Mei (Mwezi wa 5) au Juni (Mwezi wa 6) kulingana na kalenda ya wakati wetu, nayo majira ya kiangazi yalikuwa yameanza. Mashamba katika eneo hilo yalikuwa yamejaa ngano iliyokuwa tayari kuvunwa. Umati uliokuwa umekusanyika ulinyamaza. Samweli angeweza kufikia mioyo yao jinsi gani?

Watu hawakuelewa uzito wa hali iliyowakabili. Walikuwa wamesisitiza kuwa na mfalme wa kibinadamu. Hawakujua kwamba walikuwa wanaonyesha ukosefu mkubwa wa heshima kwa Mungu wao, Yehova, na kwa nabii wake pia. Kwa kweli, walikuwa wanamkataa Yehova kuwa Mfalme wao! Samweli angewasaidia jinsi gani watubu?

Samweli alizungumza nao akisema: “Mimi nimezeeka nami nina mvi.” Nywele zake nyeupe zilifanya maneno yake yawe na uzito zaidi. Kisha akasema: “Nimetembea mbele yenu tangu ujana wangu mpaka leo hii.” (1 Samweli 11:14, 15; 12:2) Ingawa Samweli alikuwa amezeeka hakuwa amesahau siku za ujana wake. Bado alikuwa anakumbuka siku hizo. Maamuzi aliyofanya wakati huo akiwa kijana, yalifanya awe na imani na kujitoa kwa Mungu wake, Yehova, katika maisha yake.

Samweli alihitaji kuendelea kusitawisha na kudumisha imani yake, ingawa alizungukwa na watu waliokosa imani na wasio waaminifu. Hata leo, si rahisi kusitawisha imani, kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu usio na imani na uliopotoka. Hebu tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa Samweli, kuanzia wakati alipokuwa mvulana mdogo.

‘Alihudumu Mbele za Yehova Akiwa Mvulana’

Maisha ya utotoni ya Samweli hayakuwa ya kawaida. Muda mfupi baada ya kuachishwa kunyonya, labda akiwa na miaka minne hivi, alianza kutumika katika maskani au hema la kukutania la Yehova huko Shilo, lilokuwa umbali wa zaidi ya kilomita 30 kutoka nyumbani kwao, Rama. Wazazi wake Elkana na Hana, walimweka wakfu kwa Yehova kwa ajili ya utumishi wa pekee na hivyo kumfanya kuwa Mnadhiri katika maisha yake yote. a Je, hilo lilimaanisha kuwa wazazi wa Samweli hawakumpenda wala hawakutaka kumtunza?

Hapana! Walijua kuwa mwana wao angetunzwa huko Shilo. Bila shaka, Kuhani Mkuu Eli alihakikisha kwamba Samweli ametunzwa vizuri kwa kuwa alifanya kazi karibu naye. Pia, kulikuwa na wanawake kadhaa waliofanya kazi fulani katika hema la kukutania, na yaelekea walifanya kazi hiyo kwa utaratibu.—Kutoka 38:8.

Zaidi ya hayo, Hana na Elkana hawakumsahau mtoto wao wa kwanza mpendwa, ambaye kuzaliwa kwake kulitokana na kujibiwa kwa sala ya Hana. Hana alikuwa amemwomba Mungu mtoto wa kiume, na kuahidi kuwa angemtoa ili amtumikie Mungu katika utumishi mtakatifu maisha yake yote. Kila mwaka, Hana alipomtembelea Samweli alimletea koti jipya lisilo na mikono, ambalo angetumia katika utumishi wake katika hema la kukutania. Kwa kweli, kijana huyo mdogo alifurahi sana mama yake alipomtembelea. Bila shaka, Samweli alifanikiwa kwa sababu wazazi wake wenye upendo walimtia moyo na kumwongoza walipomfundisha kwamba lilikuwa pendeleo kubwa kumtumikia Yehova katika sehemu hiyo ya kipekee.

Leo, wazazi wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa Hana na Elkana. Wazazi wanapowalea watoto wao, ni jambo la kawaida kukazia fikira mahitaji ya kimwili huku wakipuuza mahitaji ya kiroho ya watoto hao. Lakini wazazi wa Samweli walitanguliza mambo ya kiroho, na hilo lilichangia sana sifa ambazo mwana wao Samweli angekuwa nazo akiwa mtu mzima.—Methali 22:6.

Alipokuwa akiendelea kukua, unaweza kuwazia kijana huyo akitembea huku na huku kujionea milima iliyozunguka Shilo. Alipotazama mji huo kutoka mlimani na pia kutazama bonde lililokuwa upande mmoja wa mji huo, yaelekea moyo wake ulijawa na furaha hasa alipoona hema la kukutania la Yehova. Kwa kweli, hema hilo lilikuwa ni mahali patakatifu. b Lilikuwa limejengwa miaka 400 hivi iliyopita chini ya mwongozo wa Musa, na lilikuwa mahali pa ibada safi ya Yehova duniani kote.

Kijana Samweli alipenda hema la kukutania. Tunasoma hivi katika simulizi aliloandika baadaye: “Samweli alikuwa akihudumu mbele za Yehova, akiwa mvulana, amejifunga efodi ya kitani.” (1 Samweli 2:18) Koti hilo la kitani linaonyesha wazi kuwa Samweli aliwasaidia makuhani ndani ya hema la kukutania. Ingawa Samweli hakuwa wa jamii ya kikuhani, alikuwa na majukumu yaliyotia ndani kufungua milango ya ua wa hema la kukutania kila asubuhi na kumsaidia Eli aliyekuwa mzee kwa umri. Samweli alifurahia pendeleo hilo, hata hivyo, baada ya muda alianza kutaabika moyoni. Kulikuwa na jambo baya sana lililokuwa likiendelea ndani ya nyumba ya Yehova.

Samweli Hakuathiriwa na Upotovu Uliomzunguka

Alipokuwa na umri mdogo, Samweli alijionea upotovu na uovu mkubwa uliofanywa waziwazi. Eli alikuwa na wana wawili, Hofni na Finehasi. Simulizi la Samweli linasema: “Wana wa Eli walikuwa watu wasiofaa kitu; hawakumtambua Yehova.” (1 Samweli 2:12) Mawazo mawili yaliyo katika mstari huo yanapatana. Hofni na Finehasi walikuwa “watu wasiofaa kitu” kwa kuwa hawakumheshimu Yehova. Hawakufikiria kamwe kanuni na sheria zake za uadilifu. Jambo hilo lilikuwa chanzo kikuu cha dhambi walizotenda.

Sheria ya Mungu ilitaja waziwazi kazi za makuhani na jinsi walivyopaswa kutoa dhabihu katika madhabahu. Mungu alifanya hivyo kwa sababu nzuri! Dhabihu hizo ziliwakilisha mpango wa Mungu wa kusamehe dhambi ili watu wawe safi machoni pake, na kustahili kupata baraka na mwongozo wake. Lakini Hofni na Finehasi waliwaongoza makuhani wenzao kutoheshimu dhabihu zilizokuwa zikitolewa. c

Hebu wazia jinsi kijana Samweli alivyotazama uovu huo mkubwa uliokuwa ukiendelea bila kurekebishwa. Aliona watu wangapi—kutia ndani watu wapole, maskini, na waliokandamizwa—wakija katika hema takatifu la kukutania huku wakitumaini kufarijiwa na kutiwa moyo, lakini badala yake kuondoka wakiwa wamevunjika moyo, wameumia, au kuaibishwa? Na wazia jinsi alivyohisi alipotambua kuwa Hofni na Finehasi hawakutii sheria za Yehova kuhusu ngono, kwa kuwa walikuwa na uhusiano wa kingono na wanawake fulani waliokuwa wakitumika katika hema la kukutania? (1 Samweli 2:22) Huenda alitazamia Eli angechukua hatua fulani kuhusu jambo hilo.

Eli alikuwa na uwezo wa kutatua tatizo hilo lililokuwa linazidi kuwa baya. Akiwa kuhani mkuu, alikuwa na jukumu la kusimamia kila kitu kilichokuwa kikitendeka katika hema la kukutania. Pia akiwa baba, alikuwa na jukumu la kuwarekebisha watoto wake. Mambo hayo mabaya yaliwaumiza wao wenyewe na watu wengine wengi katika nchi hiyo. Hata hivyo, Eli alishindwa kutimiza majukumu yake, akiwa baba na akiwa kuhani mkuu. Aliwakaripia watoto wake kwa unyonge tu. (1 Samweli 2:23-25) Lakini watoto wake walihitaji nidhamu kali zaidi. Walikuwa wakitenda dhambi zilizostahili kifo!

Hali hiyo ilizidi kuwa mbaya mpaka Yehova akatuma ujumbe mzito wa hukumu kwa Eli kupitia “mtu wa Mungu,” yaani, nabii fulani ambaye hatajwi jina. Yehova alimwambia Eli hivi: “Unaendelea kuwaheshimu wana wako kuliko mimi.” Hivyo, Mungu akatabiri kuwa wana waovu wa Eli wangekufa wote wawili siku moja na familia ya Eli ingeteseka sana, na hata kupoteza pendeleo la kuwa makuhani. Je, onyo hilo kali lilileta badiliko lolote katika familia hiyo? Simulizi hilo linaonyesha kwamba familia ya Eli haikubadilika.—1 Samweli 2:27–3:1.

Upotovu huo wote ulimwathiri Samweli jinsi gani? Ingawa hali ilikuwa mbaya, bado simulizi hilo linataja mambo fulani mazuri, yaani, habari njema kuhusu ukuzi na maendeleo ya Samweli. Kumbuka kuwa kitabu cha 1 Samweli 2:18 kinasema kwamba Samweli alikuwa “akihudumu mbele za Yehova, akiwa mvulana.” Hata katika umri huo mchanga, Samweli alitumia maisha yake kumtumikia Mungu. Katika mstari wa 21 tunasoma jambo lingine lenye kutia moyo hata zaidi: ‘Mvulana Samweli aliendelea kukua akiwa na Yehova.’ Kadiri alivyoendelea kukua, ndivyo uhusiano wake na Baba yake wa mbinguni ulivyoimarika. Uhusiano huo wa kibinafsi pamoja na Yehova, ndio ulinzi hakika dhidi ya upotovu wowote.

Ingekuwa rahisi kwa Samweli kusema kwamba ikiwa kuhani mkuu na watoto wake wanaweza kufanya dhambi, hata yeye anaweza kufanya jambo lolote lile alilotaka. Lakini, upotovu unaotendwa na wengine, kutia ndani wale wenye mamlaka, si sababu ya kutenda dhambi. Leo vijana wengi Wakristo wanaiga mfano wa Samweli na ‘kuendelea kukua wakiwa na Yehova’—hata ikiwa watu wanaowazunguka hawawawekei mfano mzuri.

Samweli alifaidika jinsi gani kwa kuishi maisha ya aina hiyo? Tunasoma hivi: “Na wakati huo wote mvulana Samweli alikuwa akiendelea kukua na kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.” (1 Samweli 2:26) Kwa hiyo, Samweli alipendwa na watu ambao walikuwa na maoni yanayofaa. Yehova mwenyewe alimpenda na kumtunza kijana huyo kwa sababu ya uaminifu wake. Samweli alikuwa na hakika kuwa Mungu angechukua hatua ya kumaliza uovu uliokuwa ukiendelea huko Shilo, lakini huenda alijiuliza Mungu angefanya hivyo wakati gani.

“Sema, kwa Maana Mtumishi Wako Anasikiliza”

Usiku mmoja swali hilo lilijibiwa. Asubuhi ilikuwa inakaribia lakini bado kulikuwa na giza; nuru ya taa kubwa ya hema ilikuwa bado inaangaza. Wakati huo, Samweli akasikia sauti ikiita jina lake. Alifikiri kuwa alikuwa akiitwa na Eli, ambaye wakati huo alikuwa mzee sana na hakuwa anaona vizuri. Samweli aliamka na ‘kukimbia’ kwa mzee huyo. Je, unaweza kuwazia akilini, mvulana huyo akikimbia bila viatu ili kujua Eli alihitaji nini? Inatia moyo sana kuona kwamba Samweli alimheshimu na kumtendea Eli kwa fadhili. Ingawa Eli alikuwa akitenda dhambi, bado alikuwa kuhani mkuu wa Yehova.—1 Samweli 3:2-5.

Samweli alimwamsha Eli na kusema: “Mimi hapa, kwa maana umeniita.” Lakini Eli akasema kwamba hakuwa amemwita na akamwambia arudi kulala. Jambo hilo lilitendeka tena na tena! Mwishowe, Eli akatambua kilichokuwa kikiendelea. Muda ulikuwa umepita tangu Yehova alipotuma maono au ujumbe wa kinabii kwa watu, na haikuwa vigumu kujua ni kwa nini. Lakini Eli alijua kwamba Yehova alikuwa akizungumza tena—wakati huu kupitia Samweli! Eli alimwambia arudi kulala na akamweleza jinsi ya kujibu atakapoitwa tena. Samweli alitii. Punde si punde, akasikia sauti ikiita: “Samweli, Samweli!” Naye akajibu: “Sema, kwa maana mtumishi wako anasikiliza.”—1 Samweli 3:1, 5-10.

Angalau sasa Yehova alikuwa na mtumishi huko Shilo ambaye alikuwa anamsikiliza. Naye Samweli akawa mtu aliyemsikiliza Yehova nyakati zote. Namna gani wewe? Si lazima tungojee sauti isiyo ya kawaida itokee usiku kuzungumza nasi. Leo, sikuzote sauti ya Mungu huongea nasi kwa njia fulani. Sauti hiyo inapatikana katika Neno lake lililokamilika, Biblia. Kadiri tunavyoendelea kumsikiliza Mungu na kutenda kulingana na yale anayotuambia, ndivyo imani yetu inavyoongezeka. Hivyo ndivyo ilivyotokea kwa Samweli.

Usiku huo ulikuwa wa maana sana katika maisha ya Samweli, kwa sababu alianza kumjua Yehova katika njia ya kipekee na akawa nabii na msemaji wake. Mwanzoni, mvulana huyo aliogopa kumpa Eli ujumbe wa Yehova, kwa sababu ulikuwa tangazo la mwisho la kwamba unabii uliohusu familia hiyo ungetimizwa. Lakini Samweli alizungumza na Eli kwa ujasiri, naye Eli akakubali kwa unyenyekevu hukumu hiyo ya Mungu. Muda si muda, kila kitu ambacho Yehova alisema kilitimizwa. Waisraeli walipigana na Wafilisti, na Hofni na Finehasi wakauawa siku hiyohiyo. Naye Eli akafa baada ya kujua kuwa Sanduku takatifu la Agano lilikuwa limetekwa.—1 Samweli 3:10-18; 4:1-18.

Lakini sifa nzuri za Samweli akiwa nabii mwaminifu wa Mungu zilizidi kuongezeka. Simulizi hilo linasema, “Yehova akawa pamoja naye,” na kuongezea kuwa Yehova aliendelea kutimiza kila unabii ambao Samweli alitoa.—1 Samweli 3:19.

‘Samweli Alimwita Yehova’

Hata hivyo, je, hilo linamaanisha kwamba Waisraeli walifuata mwongozo wa Samweli na kuwa watu wa kiroho na waaminifu? Hapana. Baada ya muda, waliamua kuwa hawakutaka kuongozwa na nabii tu. Walitaka kuwa kama mataifa mengine na kutawaliwa na mfalme wa kibinadamu. Kwa mwongozo wa Yehova, Samweli alifanya kama walivyotaka. Lakini alihitaji kuwaonyesha Waisraeli uzito wa dhambi yao. Hawakuwa wanamkataa mwanadamu tu, bali Yehova mwenyewe! Kwa hiyo akawaita Waisraeli huko Gilgali.

Acheni tuone jinsi alivyozungumza na Waisraeli huko Gilgali wakati huo mgumu. Samweli aliwakumbusha Waisraeli kuhusu maisha yake ya uaminifu. Kisha, tunasoma hivi: “Samweli akamwita Yehova.” Akamwomba alete ngurumo na mvua.—1 Samweli 12:17, 18.

Kwa nini alete ngurumo na mvua wakati wa kiangazi? Hilo ni jambo lisilowezekana! Kama watu walikuwa na shaka yoyote au walimdhihaki Samweli, hawakufanya hivyo kwa muda mrefu. Ghafla mawingu meusi yalitanda angani. Upepo ukaanza kuvuma, na kuharibu ngano shambani. Nayo radi ikatoa ngurumo kwa kishindo. Na mvua ikanyesha. Watu walifanya nini? ‘Waliwaogopa sana Yehova na Samweli.’ Mwishowe, wakatambua uzito wa dhambi yao.—1 Samweli 12:18, 19.

Yehova, Mungu wa Samweli ndiye aliyefikia mioyo yao yenye kuasi, bali si Samweli. Samweli aliweka imani yake kwa Mungu tangu alipokuwa kijana hadi alipozeeka. Na Yehova alimbariki. Hata leo, Yehova hajabadilika. Bado huwategemeza wale wanaoiga imani ya Samweli.

[Maelezo ya Chini]

a Wanadhiri walikuwa chini ya nadhiri iliyowakataza kunywa vileo na kunyoa nywele zao. Wengi wao walikuwa Wanadhiri kwa muda fulani hususa, lakini wachache kati yao kama Samsoni, Samweli, na Yohana Mbatizaji, walikuwa Wanadhiri katika maisha yao yote.

b Mahali patakatifu palikuwa ni hema kubwa la kukutania lenye umbo la mstatili (rectangle), lililoshikiliwa kwa viunzi vya mbao. Hata hivyo, hema hilo lilikuwa limetengenezwa kwa vitu bora sana, yaani, ngozi ya sili, vitambaa vilivyopambwa vizuri, na mbao za bei ya juu zilizofunikwa kwa fedha na dhahabu. Mahali hapo patakatifu palizungukwa na ua. Ndani ya ua huo palikuwa pia na madhabahu yenye kupendeza ya kutolea dhabihu. Baadaye, yaelekea vyumba vingine vilivyotumiwa na makuhani vilijengwa kandokando ya hema hilo. Huenda Samweli alilala ndani ya mojawapo ya vyumba hivyo.

c Simulizi hilo linatoa mifano miwili inayoonyesha jinsi walivyokosa heshima. Kwanza, Sheria ilitaja kihususa vipande vya nyama vilivyotolewa dhabihu ambavyo makuhani waliruhusiwa kula. (Kumbukumbu la Torati 18:3) Lakini katika hema la kukutania, makuhani hao waovu walifanya jambo tofauti kabisa. Waliwalazimisha wahudumu wao kuingiza uma mkubwa ndani ya chungu cha kupikia ambacho kilikuwa na nyama zilizokuwa zikitokota, na kutoa kipande chochote kizuri walichopata! Pia, watu walipoleta dhabihu zao ili ziteketezwe juu ya madhabahu, makuhani hao waovu waliwatuma wahudumu wao kuwasumbua watu walioleta dhabihu kwa kuwaambia wawape nyama mbichi kabla ya kumtolea Yehova dhabihu ya sehemu ya mafuta.—Mambo ya Walawi 3:3-5; 1 Samweli 2:13-17.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Ingawa Samweli aliogopa, bado alimweleza Eli kuhusu ujumbe wa hukumu ambao Yehova alitoa

[Picha katika ukurasa wa 18]

Samweli alisali akiwa na imani, naye Yehova akajibu kwa kuleta ngurumo na mvua