Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Unavyoweza Kuzuia Hisia Zisizofaa

Jinsi Unavyoweza Kuzuia Hisia Zisizofaa

Jinsi Unavyoweza Kuzuia Hisia Zisizofaa

JE, WEWE unapambana na hisia zisizofaa? Bila shaka, sote tunakabili hisia hizo. Leo kuna matatizo ya kiuchumi, jeuri nyingi, na ukosefu wa haki unaozidi kuumiza watu wengi. Haishangazi kuwa watu wengi sana wamelemewa na hisia za huzuni, hatia, na hali ya kuhisi kuwa hawafai.

Hisia kama hizo zinaweza kuwa hatari sana. Zinaweza kufanya tusijiamini, tupoteze uwezo wa kufikiri vizuri, na hata kutunyang’anya furaha yetu. Biblia inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Tunahitaji kuwa na nguvu ili tuweze kupambana na ulimwengu huu wenye matatizo. Hivyo ni muhimu sana kudhibiti hisia zisizofaa. a

Biblia inaandaa mwongozo thabiti unaoweza kutusaidia kushinda hisia zisizofaa. Yehova Mungu, ambaye ni Muumba na Mtegemezaji wa uhai wote, hataki tushindwe na hisia zisizofaa wala tukose tumaini. (Zaburi 36:9) Acheni tuchunguze njia tatu ambazo Neno lake linaweza kutusaidia kupambana na hisia hizo.

Tambua Kwamba Mungu Anakujali

Watu fulani hufikiri kuwa Mungu ana shughuli nyingi sana hivi kwamba hawezi kukazia fikira hisia za kila mmoja wetu. Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Biblia inatuhakikishia kwamba Muumba wetu anajali sana hisia zetu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” (Zaburi 34:18) Inafariji kama nini kujua kwamba Mwenye Enzi Kuu na mweza yote yuko tayari kutusaidia tunapokabili hali ngumu!

Mungu anatujali sana. Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Anawapenda wanadamu na anawajali wanaoteseka. Kwa mfano, Waisraeli walipokuwa utumwani huko Misri miaka 3,500 hivi iliyopita, Mungu alisema: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo. Nami ninashuka ili kuwakomboa.”—Kutoka 3:7, 8.

Mungu anajua hisia zetu vizuri sana kwa sababu, “yeye ndiye aliyetufanya, wala si sisi wenyewe.” (Zaburi 100:3) Hivyo, tunapohisi kwamba wanadamu wenzetu hawatuelewi, tunaweza kuwa na hakika kuwa Mungu anatuelewa. Neno la Mungu linasema: “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Mungu ana uwezo wa kuona hata hisia zetu za ndani kabisa.

Bila shaka, Yehova anaona makosa na kasoro zetu. Lakini tunaweza kushukuru kuwa Muumba wetu mwenye upendo anasamehe. Daudi, mwandikaji wa Biblia aliyeongozwa na roho ya Mungu, alisema: “Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:13, 14) Mungu anatuona kwa njia tofauti na jinsi tunavyojiona. Yeye huzingatia sifa zetu nzuri na kupuuza sifa zile mbaya, mradi tu tunatubu dhambi zetu.—Zaburi 139:1-3, 23, 24.

Hivyo, tunapojihisi hatufai, tunahitaji kuazimia kupambana na hisia hizo. Lazima tukumbuke jinsi Mungu anavyotuona!—1 Yohana 3:20.

Sitawisha Urafiki wa Karibu na Mungu

Tunafaidika jinsi gani tunapojiona kama Mungu anavyotuona? Itakuwa rahisi kuchukua hatua nyingine inayoweza kutusaidia kushinda hisia zisizofaa, yaani, kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Mungu. Je, hilo linawezekana?

Kama Baba mwenye upendo, Yehova Mungu yuko tayari kutusaidia kusitawisha urafiki wa karibu pamoja naye. Biblia inatuhimiza hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Hebu fikiria jambo hili la hakika: Ingawa sisi ni dhaifu na wenye dhambi, bado tunaweza kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote mzima.

Mungu amejifunua mwenyewe katika Biblia ili tuweze kumjua vizuri. Kwa kuisoma Biblia kwa ukawaida, tunaweza kujifunza sifa za Mungu zenye kuvutia. b Tunapotafakari mambo tunayojifunza kumhusu, tutaendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Tutaelewa vizuri zaidi kwamba yeye kwa kweli ni Baba mwenye upendo na huruma.

Kutafakari kwa undani yale tunayojifunza katika Biblia kutatusaidia hata zaidi. Tunamkaribia Baba yetu wa mbinguni kwa kuruhusu maoni yake yaingie katika akili na mioyo yetu, na kukubali yaturekebishe, yatufariji, na kutuongoza. Tunahitaji kufanya hivyo hasa tunapopambana na mawazo na hisia zinazotusumbua au kutufadhaisha. Mtunga zaburi alisema hivi: “Mahangaiko ya moyo wangu yanapozidi, wewe wanifariji na kunifurahisha.” (Zaburi 94:19, BHN) Neno la Mungu linaweza kutufariji sana. Ikiwa tutakubali Neno la Mungu kwa unyenyekevu, huenda hisia zetu zisizofaa zikabadilika na tukapata faraja na amani ambayo Mungu pekee ndiye aliye na uwezo wa kuitoa. Hivyo, Yehova anatufariji kama mzazi mwenye upendo anavyomtuliza mtoto ambaye ameumia au kukasirika.

Jambo lingine linaloweza kutusaidia kuwa rafiki za Mungu ni kuongea naye kwa ukawaida. Biblia inatuhakikishia ya kwamba “hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, [Mungu] hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Hata tuwe na mahangaiko ya aina gani, tunaweza kumwomba Mungu atusaidie. Tukimweleza yaliyo moyoni mwetu, tunapata amani ya akili. Mtume Paulo aliandika hivi: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

Unapoendelea kufuata ratiba ya kusoma Biblia, kutafakari, na kusali kibinafsi, bila shaka, utajenga uhusiano wa karibu pamoja na Baba yako wa mbinguni. Uhusiano huo wa karibu ni silaha inayoweza kutusaidia kupambana na hisia zisizofaa. Ni jambo gani lingine linaloweza kukusaidia?

Kazia Fikira Tumaini Hakika la Wakati Ujao

Hata tukabili hali ngumu kiasi gani, bado tunaweza kukazia fikira mambo mazuri. Jinsi gani? Mungu ametupa tumaini hakika la wakati ujao. Mtume Petro alisema hivi kuhusu tumaini hilo zuri: “Kulingana na ahadi [ya Mungu] tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Hilo linamaanisha nini?

Maneno “mbingu mpya” yanamaanisha serikali, yaani, Ufalme wa mbinguni wa Mungu unaoongozwa na Yesu Kristo. “Dunia mpya” inamaanisha jamii mpya ya wanadamu iliyokubaliwa na Mungu ambayo itaishi hapa duniani. Chini ya utawala wa “mbingu mpya,” jamii mpya ya kidunia haitapatwa na mambo yanayosababisha hisia zisizofaa. Kuhusu wanadamu waaminifu watakaoishi wakati huo, Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.

Kwa kweli, hayo ni mambo yenye kuchangamsha na kutia moyo sana. Hiyo ndiyo sababu Biblia inataja kwamba ahadi za wakati ujao ambazo Mungu amewapa Wakristo wa kweli, ni “tumaini la furaha.” (Tito 2:13) Tunapokazia fikira ahadi za Mungu za wakati ujao kwa wanadamu—na sababu zinazofanya tuamini kuwa ahadi hizo zinategemeka na ni za kweli—tunayasukuma mbali mawazo yasiyofaa.—Wafilipi 4:8.

Biblia hufananisha tumaini letu la wokovu na kofia ya chuma. (1 Wathesalonike 5:8) Katika nyakati za kale, askari jeshi hangeenda vitani bila kofia ya chuma. Alijua kwamba kofia hiyo ingemzuia asiumie anapogongwa kichwani na kitu chochote kile. Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa, ndivyo tumaini linavyolinda akili. Tunapoendelea kufikiria mambo yanayotusaidia kuwa na tumaini, tunalindwa ili tusiwe na woga na mawazo yasiyofaa.

Kwa hiyo, inawezekana kushinda hisia zisizofaa. Bila shaka, hata wewe unaweza kufanya hivyo! Tafakari jinsi Mungu anavyokuona, mkaribie, na ukazie fikira tumaini lako la wakati ujao. Hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba utaishi wakati ambapo watu hawatapambana kamwe na hisia zisizofaa!—Zaburi 37:29.

[Maelezo ya Chini]

a Wale ambao wamekuwa na tatizo la kushuka moyo kwa muda mrefu wanapaswa kumwona daktari.—Mathayo 9:12.

b Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2009 (1/8/2009) lina ratiba nzuri inayoweza kukusaidia kusoma Biblia.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

“Nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.”—KUTOKA 3:7, 8

[Picha katika ukurasa wa 20]

“Mahangaiko ya moyo wangu yanapozidi, wewe wanifariji na kunifurahisha.”—ZABURI 94:19, BIBLIA HABARI NJEMA

[Picha katika ukurasa wa 21]

“Amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”—WAFILIPI 4:7

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Maandiko Yenye Kufariji Kumhusu Yehova Mungu

“Yehova, Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.”—KUTOKA 34:6.

“Macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 MAMBO YA NYAKATI 16:9.

“Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—ZABURI 34:18.

“Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe.”—ZABURI 86:5.

“Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.”—ZABURI 145:9.

“Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—ISAYA 41:13.

“Abarikiwe . . . Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 WAKORINTHO 1:3.

“Tutaihakikishia mioyo yetu mbele zake kwa habari ya lolote ambalo huenda mioyo yetu ikatuhukumu kuwa na hatia, kwa sababu Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.”—1 YOHANA 3:19, 20.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

Wamefaulu Kupambana na Hisia Zisizofaa

“Baba yangu ni mlevi wa kupindukia, na amenifanya niteseke sana. Kwa muda mrefu nimekuwa nikihisi kuwa sifai. Lakini nilipokubali kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, nilijifunza kuhusu tumaini la uzima wa milele duniani. Kwa sababu ya tumaini hilo, nilijawa na furaha akilini na moyoni mwangu. Nilianza kusoma Biblia kwa ukawaida. Mimi huwa na Biblia kila mara. Ninapoanza kuwa na hisia zisizofaa, mimi huifungua na kusoma maandiko yenye kutia moyo. Kusoma kuhusu sifa zenye kuvutia za Mungu hunihakikishia jinsi nilivyo na thamani machoni pake.”—Kátia, mwanamke mwenye umri wa miaka 33. c

“Nilikuwa mlevi kupindukia, mraibu wa bangi, kokeini, kokeini kali, na nilinusa gundi. Baada ya kupoteza kila kitu nilichokuwa nacho, nilianza kuomba-omba. Lakini baada ya kukubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilibadili maisha yangu kabisa. Nikawa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Ingawa bado mimi ninapambana na hali ya kujihisi nina hatia au sifai, nimejifunza kutegemea rehema na fadhili zenye upendo za Mungu. Nina hakika kuwa Mungu ataendelea kunipa nguvu za kushinda hisia zisizofaa. Kujua kweli za Biblia ndilo jambo zuri zaidi kuwahi kutukia maishani mwangu.”—Renato, mwanamume mwenye umri wa miaka 37.

“Tangu nilipokuwa kijana mdogo, nilikuwa nikijilinganisha na ndugu yangu mkubwa. Nilijihisi duni mbele zake. Bado mimi hujihisi siko salama na sijiamini. Lakini nimeazimia kushinda pambano hilo. Nimesali kwa Yehova bila kuacha, naye amenisaidia kushinda hali ya kujihisi sifai. Inatia moyo kama nini kujua kuwa Mungu ananipenda na ananijali kikweli!”—Roberta, mwanamke mwenye umri wa miaka 45.

[Maelezo ya Chini]

c Baadhi ya majina yamebadilishwa.