Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwezo wa Kusema kwa Lugha Je, Unatoka kwa Mungu?

Uwezo wa Kusema kwa Lugha Je, Unatoka kwa Mungu?

Uwezo wa Kusema kwa Lugha Je, Unatoka kwa Mungu?

“SIELEWI,” anasema Devon. “Kila juma, watu wengi katika kanisa langu huonekana kupokea roho takatifu na kusema kwa lugha mbalimbali kimuujiza. Baadhi yao wanaishi maisha mapotovu. Mimi hujitahidi kuishi kupatana na kanuni za Biblia. Lakini hata nisali kwa bidii kadiri gani, mimi sipati zawadi hiyo ya roho. Kwa nini iwe hivyo?”

Gabriel naye ni mshiriki wa kanisa ambalo waumini wake huonekana kupokea roho takatifu na kusema kwa lugha mbalimbali. Yeye anasema, “Jambo linalonisumbua ni moja. Wakati ninaposali, watu wengine hunikatiza kwa sala wanazotoa kwa sauti kubwa wakitumia maneno ambayo siyaelewi wala wao wenyewe hawayaelewi. Hakuna mtu ambaye hufaidika na sala hizo. Lakini ikiwa zawadi inatokana na roho ya Mungu, si inapaswa kuwa na manufaa?”

Mambo ambayo Devon na Gabriel wamejionea yanatokeza swali lenye kuamsha fikira, Je, ni kweli kwamba uwezo wa kusema kwa lugha, kama ilivyo katika makanisa fulani leo, unatoka kwa Mungu? Ili kujibu swali hilo, inafaa kuchunguza jinsi zawadi ya kimuujiza ya kuzungumza kwa lugha ilivyotumiwa kati ya Wakristo wa karne ya kwanza.

‘Walianza Kusema kwa Lugha Mbalimbali’

Katika Biblia, tunasoma kuhusu wanaume na wanawake fulani ambao walipewa uwezo wa kuzungumza kwa lugha ambazo hawakuwa wamewahi kujifunza. Hilo lilitukia kwa mara ya kwanza siku ya Pentekoste 33 W.K., majuma kadhaa baada ya kifo cha Yesu Kristo. Wanafunzi 120 hivi waliokuwa Yerusalemu siku hiyo ‘walijazwa roho takatifu wakaanza kusema katika lugha tofauti.’ Watu kutoka nchi za kigeni ‘walishikwa na bumbuazi, kwa sababu kila mmoja aliwasikia wakisema katika lugha yake mwenyewe.’—Matendo 1:15; 2:1-6.

Biblia pia inataja wafuasi wengine wa Yesu wa karne ya kwanza ambao walikuwa na uwezo huo wa kipekee. Kwa mfano, kwa nguvu za roho takatifu, mtume Paulo aliweza kuzungumza kwa lugha mbalimbali kimuujiza. (Matendo 19:6; 1 Wakorintho 12:10, 28; 14:18) Lakini zawadi kama hiyo ya roho takatifu ya Mungu inapaswa kutolewa kwa kusudi zuri. Kwa hiyo, ni kwa kusudi gani watu katika nyakati za Biblia walipewa uwezo wa kusema kwa lugha mbalimbali?

Ishara ya Kuungwa Mkono na Mungu

Alipowaandikia Wakristo katika jiji la Korintho, ambao baadhi yao wangeweza kuzungumza kwa lugha mbalimbali, Paulo alieleza kwamba “lugha ni kwa ajili ya ishara . . . kwa wasio waamini.” (1 Wakorintho 14:22) Kwa hiyo, uwezo wa kusema kwa lugha, kutia ndani uwezo mbalimbali wa kufanya miujiza, ulikuwa ishara kwa watazamaji kwamba Mungu alilikubali na kuliunga mkono kutaniko jipya la Kikristo lililokuwa limefanyizwa. Zawadi za kimuujiza zilikuwa kama ishara za barabarani ambazo ziliwaelekeza watu waliokuwa wakitafuta kweli wafike mahali walipopaswa kwenda, ili kuwapata watu waliochaguliwa na Mungu.

Ni muhimu kutambua kwamba Biblia haisemi kuwa Yesu wala nabii yeyote wa kabla ya Ukristo alikuwa na uwezo wa kimuujiza wa kusema kwa lugha ambazo hawakuzijua. Basi, ni wazi kwamba kuna sababu nyingine iliyofanya wanafunzi wa Yesu wapewe zawadi ya kusema kwa lugha mbalimbali.

Zawadi ya Kusema kwa Lugha Yatumiwa Kueneza Habari Njema

Mapema katika huduma yake, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wahubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu kwa Wayahudi tu. (Mathayo 10:6; 15:24) Kwa sababu hiyo, wanafunzi walihubiri hasa katika maeneo yaliyokuwa na Wayahudi wengi. Lakini muda si muda, mambo yangebadilika.

Muda mfupi baada ya kifo chake mwaka wa 33 W.K., Yesu aliyefufuliwa aliwaamuru wafuasi wake ‘wakafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ Pia, aliwaambia wafuasi wake kwamba wangekuwa mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mathayo 28:19; Matendo 1:8) Ili kueneza habari njema kwa kiwango hicho, wanafunzi wangehitaji kutumia lugha nyingine nyingi kando na Kiebrania.

Hata hivyo, wengi kati ya wanafunzi hao wa mapema walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Matendo 4:13) Hivyo basi, wangewezaje kuhubiri katika nchi za mbali ambako watu walizungumza lugha ambazo hawajawahi kuzisikia wala kuzizungumza? Roho takatifu iliwapa baadhi ya wahubiri hao wenye bidii uwezo wa kimuujiza wa kuhubiri kwa ufasaha katika lugha ambazo hawakuzijua.

Kwa hiyo, zawadi ya kusema kwa lugha ilitolewa kwa malengo mawili muhimu. Kwanza, ilikuwa ishara kwamba Mungu aliliunga mkono kutaniko la Kikristo. Pili, ilisaidia sana Wakristo wa karne ya kwanza kutimiza utume wao wa kuwahubiria watu wa lugha mbalimbali. Je, wale wanaosema kwa lugha katika makanisa mbalimbali leo wanatimiza malengo hayo?

Kusema kwa Lugha Leo, Je, Ni Ishara ya Kuungwa Mkono na Mungu?

Ungeweka ishara wapi ili kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo katika eneo lako? Ndani ya jengo dogo? Hapana! Simulizi kuhusu siku ya Pentekoste linasema kuwa “umati” wa wapita-njia waliona ishara wakati wanafunzi walipozungumza kwa lugha mbalimbali kimuujiza. Kwa sababu hiyo, “nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa” katika kutaniko la Kikristo siku hiyo! (Matendo 2:5, 6, 41) Ikiwa leo watu wanaodai kusema kwa lugha wanafanya hivyo tu ndani ya kanisa, jambo hilo linaweza jinsi gani kuwa ishara inayoonekana waziwazi na umati wa wasioamini?

Neno la Mungu linataja uasherati na “matendo [mengine] ya mwili” kuwa yanapingana na utendaji wa roho takatifu, na kuongeza kwamba “wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Wagalatia 5:17-21) Iwapo unawaona watu wenye mwenendo mpotovu wakisema kwa lugha, huenda kwa kufaa ukauliza, ‘Je, hilo si jambo lisilowezekana—hata lenye kupotosha—kwa Mungu kuwapa roho takatifu watu walio na mazoea ya kufanya mambo ambayo yanashutumiwa na Neno lake?’ Hilo ni kama kuweka ishara ya barabarani inayopotosha watu.

Je, Kusema kwa Lugha Leo Kunatumiwa Kueneza Habari Njema?

Namna gani kuhusu lile kusudi lingine la zawadi ya kusema kwa lugha katika karne ya kwanza? Je, kusema kwa lugha katika makanisa leo kunachangia kuenezwa kwa habari njema kwa watu wa lugha mbalimbali? Kumbuka kwamba watazamaji waliokuwa Yerusalemu siku ya Pentekoste 33W.K., walitoka katika nchi nyingi, na walielewa vizuri lugha zilizozungumzwa kimuujiza na wanafunzi. Tofauti na hilo wale wanaosema kwa lugha leo, kwa kawaida husema mambo yasiyoweza kueleweka na yeyote.

Bila shaka, wale wanaosema kwa lugha leo wanafanya hivyo kwa njia tofauti kabisa na jinsi wafuasi wa mapema wa Yesu waliopewa zawadi ya roho takatifu walivyofanya. Hata hakuna uthibitisho wenye kutegemeka kwamba kuna yeyote aliyepokea nguvu hizo za kimuujiza baada ya mitume kufa. Jambo hilo haliwashangazi wasomaji wa Biblia. Kuhusu zawadi za kimuujiza, kutia ndani kusema kwa lugha, mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kutabiri hivi: “Zitakoma.” (1 Wakorintho 13:8) Hivyo basi, tunaweza kujua jinsi gani kwamba mtu ana roho takatifu leo?

Ni Nani kwa Kweli Wana Roho Takatifu Leo?

Yesu alijua kwamba zawadi ya kusema kwa lugha mbalimbali ingekoma muda mfupi baada ya kufanyizwa kwa kutaniko la Kikristo. Punde kabla ya kifo chake, Yesu alitaja ishara yenye kudumu ambayo ingewatambulisha wafuasi wake wa kweli. Alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Katika ule mstari ambapo Neno la Mungu linatabiri kuwa zawadi za kimuujiza zingekoma hatimaye, tunasoma: “Upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:8.

Upendo umeorodheshwa wa kwanza kati ya sehemu tisa za “matunda” ya roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hiyo, wale ambao kwa kweli wana roho ya Mungu—na hivyo wanaungwa mkono na Mungu—wangependana kikweli. Zaidi ya hayo, sehemu ya tatu ya matunda ya roho ni amani. Kwa hiyo, wale walio na roho takatifu leo wangekuwa watu wenye kujitolea kudumisha amani, wanaojitahidi sana kuepuka mambo kama imani kali, ubaguzi, na ujeuri.

Pia, kumbuka unabii wa Yesu katika Matendo 1:8. Alitabiri kwamba wanafunzi wake wangepokea nguvu ili wawe mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” Yesu pia alisema kwamba kazi hiyo ingeendelea “hata mwisho wa dunia.” (Mathayo 28:20, Zaire Swahili Bible) Hivyo, kazi hii ya kuhubiri duniani kote ingeendelea kuwa ishara ya kuwatambulisha wale ambao kwa kweli wana nguvu ya roho takatifu.

Una maoni gani? Ni kikundi gani cha watu ambacho unaona kwa kweli kina roho takatifu leo? Ni nani wanaoonyesha matunda ya roho, hasa upendo na amani, kiasi kwamba wanateswa na serikali kwa sababu wanakataa kupigana vita katika jeshi lolote duniani? (Isaya 2:4) Ni nani wanaojitahidi kuepuka kazi za mwili, kama vile uasherati, na hata kuwaondoa kati yao watu wenye mazoea hayo ambao hawatubu? (1 Wakorintho 5:11-13) Ni nani wanaohubiri ulimwenguni kote habari njema kwamba Ufalme wa Mungu ndilo tumaini pekee kwa wanadamu?—Mathayo 24:14.

Wachapishaji wa gazeti hili hawana shaka kusema kwamba Mashahidi wa Yehova ndio watu ambao, kupatana na maelezo ya Biblia, wana roho takatifu. Tunakutia moyo uwajue vizuri zaidi na ujiamulie mwenyewe kama kwa kweli wanaungwa mkono na Mungu.