Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Musa​—Alikuwa Mnyenyekevu Sana

Musa​—Alikuwa Mnyenyekevu Sana

UNYENYEKEVU NI NINI?

Unyenyekevu unamaanisha kutokuwa na kiburi wala majivuno. Mtu mnyenyekevu hajioni kuwa bora kuliko wengine. Mwanadamu asiye mkamilifu na ambaye ni mnyenyekevu anapaswa pia kuwa na kiasi, yaani, kutambua mipaka yake.

MUSA ALIONYESHAJE UNYENYEKEVU?

Musa hakujivuna alipopata mamlaka. Kwa kawaida, mtu hutambulika kama ni mnyenyekevu au la anapopewa mamlaka fulani. Mwandishi wa karne ya kumi na tisa Robert G. Ingersoll alisema hivi: “Watu wengi wanaweza kustahimili shida. Lakini ikiwa unataka kujua jinsi mtu alivyo kikweli, mpe mamlaka.” Kuhusiana na mamlaka, Musa aliweka mfano bora wa unyenyekevu. Jinsi gani?

Musa alipewa mamlaka kubwa, kwa sababu Yehova alimwagiza awaongoze Waisraeli. Hata hivyo, mamlaka hayo hayakumfanya Musa awe na kiburi. Kwa mfano, fikiria jinsi alivyoshughulikia tatizo gumu kuhusu haki za urithi. (Hesabu 27:1-11) Lilikuwa jambo gumu, kwa sababu maamuzi hayo yangeathiri hata vizazi vilivyofuata.

Musa alifanya nini? Je, alifikiria kwamba akiwa kiongozi wa Israeli, alijua uamuzi aliopaswa kufanya? Je, alitegemea uwezo wake binafsi, uzoefu wake, au ujuzi wake kumhusu Yehova?

Huenda mtu mwenye kiburi angefanya hivyo. Lakini Musa alitenda tofauti. Biblia inasema hivi: “Musa akaiweka kesi yao mbele za Yehova.” (Hesabu 27:5) Hebu fikiria! Hata baada ya kuwaongoza Waisraeli kwa miaka 40, bado Musa alimtegemea Yehova. Mfano huo unaonyesha wazi kwamba Musa alikuwa mnyenyekevu.

Musa hakufikiria ni yeye tu aliyepaswa kuwa na mamlaka. Alishangilia Yehova aliporuhusu Waisraeli wengine kutenda kama manabii pamoja naye. (Hesabu 11:24-29) Baba-mkwe wake alipopendekeza kwamba achague watu ambao wangemsaidia kufanya kazi, Musa alifuata ushauri huo kwa unyenyekevu. (Kutoka 18:13-24) Alipokaribia mwisho wa maisha yake, ingawa bado alikuwa mwenye nguvu, Musa alimwomba Yehova achague mtu ambaye angeongoza baada yake. Yehova alipomchagua Yoshua, Musa alimuunga mkono mwanamume huyo, na akawasihi watu wafuate mwongozo wa Yoshua ili kuingia kwenye Nchi ya Ahadi. (Hesabu 27:15-18; Kumbukumbu la Torati 31:3-6; 34:7) Kwa kweli, Musa alithamini pendeleo la kuwaongoza Waisraeli katika ibada ya kweli. Hata hivyo, hakutumia mamlaka yake kuwakandamiza watu wengine.

TUNAJIFUNZA NINI?

Hatupaswi kuruhusu uwezo, mamlaka, wala vipawa vyetu vifanye tuwe na kiburi. Kumbuka: Ili tumtumikie Yehova kwa njia inayofaa unyenyekevu ni muhimu kuliko uwezo wetu. (1 Samweli 15:17) Ikiwa sisi ni wanyenyekevu kikweli, tutajitahidi kutumia ushauri huu wa Biblia wenye hekima: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.”—Methali 3:5, 6.

Mfano wa Musa unatufundisha pia kwamba hatupaswi kukazia fikira kupita kiasi cheo au mamlaka yetu.

Je, tunafaidika kwa kuiga unyenyekevu wa Musa? Bila shaka! Tunapositawisha unyenyekevu wa kweli tunafanya watu walio karibu nasi wastarehe, na inakuwa rahisi kwao kutupenda. Jambo muhimu zaidi ni kwamba tutapendwa na Yehova Mungu, ambaye huonyesha sifa hiyo. (Zaburi 18:35) “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.” (1 Petro 5:5) Hiyo ni sababu yenye nguvu ya kutufanya tuige unyenyekevu wa Musa!