Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KICHWA KIKUU: UFUFUO WA YESU—UNA UMUHIMU GANI KWAKO?

Ufufuo wa Yesu—Je, Kweli Ulitukia?

Ufufuo wa Yesu—Je, Kweli Ulitukia?

HERODOTO, mwanahistoria Mgiriki aliyeishi miaka 2,500 iliyopita, alisimulia kuhusu Wamisri wa siku zake. Aliandika hivi: “Katika karamu ya matajiri, baada ya chakula cha jioni mwanamume fulani hubeba jeneza lililo na sanamu ya maiti, iliyochongwa na kupakwa rangi ili ifanane kabisa na maiti, yenye urefu wa mkono mmoja au mwili. Anamwonyesha kila mtu aliyeko akisema, ‘Kunyweni na msherehekee, kwa maana; mtakapokufa mtakuwa hivi.’”

Si Wamisri peke yao waliokuwa na maoni kama hayo kuhusu uhai na kifo. Leo, msemo “Kuleni, mnywe, na msherehekee” ni wa kawaida. Ikiwa kifo ni mwisho wa uhai, kwa nini usijifurahishe? Kwa nini ujitahidi kufanya yaliyo sawa? Ikiwa kifo ni mwisho wa mambo yote, kuishi kwa ajili ya sasa kunatosha. Mtume Paulo alizungumzia jambo hilo. Alifafanua mtazamo wa watu wasioamini ufufuo akisema hivi: “Ikiwa wafu hawatafufuliwa, ‘na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.’”—1 Wakorintho 15:32.

Bila shaka, Paulo mwenyewe hakuamini kwamba wafu watasahauliwa milele. Alisadiki wafu wataishi tena, wakiwa na tumaini la kuishi milele. Usadikisho wake ulitegemea tukio kubwa na muhimu, ukweli ambao aliamini haupingiki—ufufuo * wa Kristo Yesu. Kwa hakika, ufufuo huo ni tukio kubwa la kipekee ambalo liliimarisha imani ya wanafunzi wa mapema.

Hata hivyo, ufufuo wa Yesu una umuhimu gani kwetu? Kwa kweli, tunajuaje kwamba ulitukia? Acheni tuone jinsi Paulo alivyozungumzia jambo hilo alipowaandikia Wakristo walioishi Korintho.

 INGEKUWAJE KAMA KRISTO HAKUFUFULIWA?

Wakristo fulani wa jiji la kale la Korintho walitatanishwa na jambo hilo, na wengine hawakuamini ufufuo hata kidogo. Katika barua yake ya kwanza kwa Wakristo hao, Paulo aliorodhesha mambo ambayo yangetokea ikiwa ufufuo haukuwa halisi. Aliandika hivi: “Ikiwa, kwa kweli, hakuna ufufuo wa wafu, basi Kristo hakufufuliwa. Lakini ikiwa Kristo hakufufuliwa, hakika kuhubiri kwetu ni bure, na imani yetu ni bure. Zaidi ya hayo, tunaonekana pia kuwa mashahidi wa uwongo wa Mungu . . . Imani yenu ni bure; ninyi bado mko katika dhambi zenu. . . . Pia, wale waliolala usingizi katika kifo katika muungano na Kristo waliangamia.”—1 Wakorintho 15:13-18.

“Aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mmoja . . . Baadaye alimtokea Yakobo, kisha mitume wote; lakini mwisho kabisa alinitokea mimi pia.”—1 Wakorintho 15:6-8

Paulo alianza kwa maneno ambayo hayawezi kupingwa: Ikiwa wafu hawatafufuliwa, basi, Kristo, aliyekufa hakufufuliwa. Kama Kristo hakufufuliwa ingekuwaje? Basi, kuhubiri habari njema ingekuwa kazi bure na uwongo mkubwa. Zaidi ya yote, ufufuo wa Kristo ulikuwa sehemu muhimu ya imani ya Kikristo, na haungetenganishwa na mafundisho ya msingi ya Biblia kuhusu utawala wa Mungu, jina lake, Ufalme wake, na ukombozi wetu. Ikiwa ufufuo haukutukia, ujumbe ambao Paulo na mitume wengine walitangaza ungekuwa bure kabisa, usio na thamani yoyote.

Mambo mengine yangefuata. Ikiwa Kristo hakufufuliwa kutoka kwa wafu, imani ya Kikristo ingekuwa bure, isiyo na thamani yoyote, na inayotegemea uwongo. Zaidi ya hayo, Paulo na wengine wangelikuwa wamesema uwongo si juu ya ufufuo wa Yesu pekee bali pia kumhusu yule ambaye walisema alimfufua Yesu, yaani Yehova Mungu. Zaidi ya hilo, dai la kwamba Kristo “alikufa kwa ajili ya dhambi zetu” lingekuwa la uwongo—kwa maana ikiwa Mkombozi mwenyewe hakukombolewa kutoka katika kifo, angewezaje kuwakomboa wengine? (1 Wakorintho 15:3) Hilo lingemaanisha kwamba Wakristo waliokufa, kutia ndani waliouawa kwa sababu ya imani yao, waliangamia wakiwa na tumaini la uwongo kwamba watafufuliwa.

Paulo alihitimisha hivi: “Ikiwa katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi ndio wa kusikitikiwa zaidi kati ya watu wote.” (1 Wakorintho 15:19) Kama Wakristo wengine, Paulo alipata hasara, aliteswa, akavumilia matatizo, na kuuawa kwa sababu aliamini ufufuo na yale ambayo ufufuo ungetimiza. Ingekuwa bure kabisa kama kusingekuwa na ufufuo!

KWA NINI UNAPASWA KUAMINI UFUFUO?

Paulo hakufikiri kwamba aliamini uwongo. Alijua Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu, na alimalizia uthibitisho wake kwa Wakorintho hivi, “kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alimtokea Kefa, kisha wale kumi na wawili.” * Halafu akaongeza hivi: “Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mmoja, ambao walio wengi kati yao wapo mpaka sasa, lakini wengine wamelala usingizi katika kifo. Baadaye alimtokea Yakobo, kisha mitume wote; lakini mwisho kabisa alinitokea mimi pia.”—1 Wakorintho15:3-8.

 Paulo alianza kwa maneno yenye usadikisho kwamba Kristo alikufa, akazikwa, na kufufuliwa kwa ajili ya dhambi zetu. Kwa nini Paulo alikuwa na uhakika huo? Sababu moja ni kwamba watu wengi walijionea. Yesu aliyefufuliwa aliwatokea watu mmoja mmoja (kutia ndani Paulo mwenyewe), vikundi vidogo, na hata umati wa watu 500, ambao wengi wao hawakuamini waliposikia kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa! (Luka 24:1-11) Wengi wa mashahidi hao walikuwa hai wakati wa Paulo na wangeweza kuulizwa ili kuthibitisha tukio hilo. (1 Wakorintho15:6) Ingekuwa rahisi kumpuuza shahidi mmoja au wawili, lakini si uthibitisho wa watu 500 au zaidi.

Pia, kumbuka Paulo alitaja mara mbili kwamba kufa, kuzikwa, na kufufuliwa kwa Yesu ‘kulilingana na Maandiko.’ Matukio hayo yalithibitisha kwamba unabii ulio katika Maandiko ya Kiebrania kuhusu Masihi ulikuwa wa kweli na bila shaka, Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa.

Licha ya uthibitisho wa mashahidi na Maandiko, kulikuwepo, na bado kuna watu wanaoshuku ikiwa Yesu alifufuliwa. Wengine wanasema mwili wake uliibiwa na wanafunzi wake ambao walidai kwamba walishuhudia ufufuo. Hata hivyo, wanafunzi hawakuwa na nguvu wala uwezo wa kuwashinda askari Waroma waliokuwa wanalinda kaburi. Wengine wanadai ufufuo ulikuwa jambo la kuwaziwa tu. Maoni hayo si ya kweli kwa sababu Yesu aliwatokea watu wengi kwa nyakati tofauti. Pia, je, unaweza kuamini kwamba mtu wa kuwazia angepika na kuwapa wanafunzi samaki kama Yesu aliyefufuliwa alivyofanya huko Galilaya? (Yohana 21: 9-14) Je, mtu wa kuwaziwa anaweza kuwaomba watu wamguse?—Luka 24:36-39.

 Wengine wanasema kwamba ufufuo ni uwongo uliotungwa na wanafunzi. Lakini wangepata faida gani kwa kufanya hivyo? Kutoa ushahidi kuhusu ufufuo kulifanya wanafunzi wadhihakiwe, wateswe na kuuawa. Kwa nini wahatarishe uhai kwa kuunga mkono uwongo? Zaidi ya hayo, kwanza walitoa ushahidi wao Yerusalemu, mbele ya wapinzani wao, ambao walikuwa tayari kutumia kisingizio chochote ili kuwashutumu.

Ufufuo ndilo jambo lililowapa wanafunzi ujasiri wa kutangaza juu ya Bwana wao licha ya kunyanyaswa vikali. Ukweli kuhusu ufufuo ukawa sehemu muhimu ya imani ya Kikristo. Wakristo wa mapema hawakuhatarisha uhai wao ili tu kutoa ushahidi kuhusu mwalimu mwenye hekima aliyeuawa. Walihatarisha uhai wao ili kuhubiri ufufuo wa Yesu kwa sababu ulithibitisha kwamba alikuwa Kristo, Mwana wa Mungu, mwenye nguvu, aliye hai ambaye aliwategemeza na kuwaongoza. Ufufuo wake ulimaanisha kwamba wao pia wangefufuliwa kutoka kwa wafu. Kwa kweli, kama Yesu hakufufuliwa, kusingekuwa na Ukristo. Kama Yesu hakufufuliwa, hata hatungewahi kumsikia.

Hata hivyo, ufufuo wa Kristo una umuhimu gani kwetu leo?

^ fu. 5 Katika Biblia, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ufufuo” kihalisi humaanisha “kusimama tena.” Hilo linadokeza kwamba mtu hurudishiwa uhai, akiwa na sura ileile, utu, na kumbukumbu lake.

^ fu. 13 Usemi “wale kumi na wawili” unamaanisha “mitume,” ingawa walibaki 11 baada ya Yuda Iskariote kufa. Kwenye tukio moja, 10 pekee waliwakilisha wale mitume 12, kwa kuwa Tomasi hakuwepo.—Yohana 20:24.