Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA

Dini Zimeanza Kukosa Watu?

Dini Zimeanza Kukosa Watu?

Gaffar, mwenye alizaliwa katika inchi ya Uturuki, alihangaishwa na wazo la kwamba Mungu analipiza kisasi, lenye alifundishwa katika dini yake. Hediye, bibi yake, alianza kuwa na mashaka juu ya dini yake wakati alikuwa tu na miaka 9. Alisema hivi: “Nilifundishwa kuamini kama kila kitu chenye kutufikia katika maisha kimepangwa mbele ya wakati. Kwa sababu nilikuwa yatima, nilijiuliza, ‘Nilifanya nini ili jambo hili linifikie?’ Mara nyingi, nililia usiku muzima. Kufikia miaka 15, nilikuwa nimeachana na dini yangu katika moyo wangu.”

UMEACHANA na dini fulani? Kama jibu lako ni ndiyo, hauko wewe mwenyewe. Katika inchi nyingi, hesabu ya watu wenye kusema kama ‘hawana dini’ inaendelea kuongezeka, jambo hilo linaonyesha kama haijulikane ikiwa dini itakuwa namna gani wakati unaokuja. Inchi fulani kati ya hizo zinaonyeshwa hapa chini.

Sababu Gani Watu Wanaachana na Dini?

Kuko sababu nyingi zenye kufanya watu wavunjike moyo kwa sababu ya dini. Kati ya sababu hizo kuko jeuri ao matendo ya kuogopesha yenye dini inachochea ao kuitika, matendo machafu ya uasherati yenye kufanywa na viongozi wa dini, na mambo mengine ambayo hayaonekane waziwazi yenye kufanya watu wengi zaidi waachane na dini. Mambo hayo ni kama vile:

  • Utajiri: Kichapo kimoja kinasema hivi: “Kama mutu anakuwa tajiri sana, hatahangaikia pia dini sana.” (Global Index of Religion and Atheism) Jambo lenye kichapo hicho kilisema ni la maana kwa sababu katika inchi nyingi, utajiri umeongezeka sana. Kulingana na John Nye, profesa wa mambo ya feza, katika maeneo fulani watu wanaishi “maisha yenye ingefanya mufalme mukubwa mwenye aliishi miaka mia mbili iliyopita atamani sana utajiri wao.”

    MAMBO BIBLIA INASEMA: Biblia ilitabiri kama katika “siku za mwisho,” watu watapenda feza kuliko kupenda Mungu na jirani. (2 Timotheo 3:1-5) Muandikaji mumoja wa Biblia alijua hatari yenye kuletwa na utajiri, kwa hiyo, alimuambia Yehova Mungu hivi: ‘Usinipe umasikini wala utajiri.’ Sababu gani aliomba hivyo? Aliongeza hivi: “Nisije nikashiba nikakukana.”—Methali 30:8, 9.

  • Desturi za dini na mwenendo: Watu wengi, zaidi sana vijana, wanaona kuwa dini haina faida leo.Wengine hawatumainie tena dini. Tim Maguire, musimamizi wa vyombo vya habari wa shirika moja katika inchi ya Écosse (Humanist Society Scotland), alisema hivi: “Kama unaangalia namna dini zimejiendesha kwa mamia ya miaka, watu wameachana nazo kwa sababu hawaamini tena kuwa ziko na mamlaka ya kutoa mashauri juu ya mwenendo.”

    MAMBO BIBLIA INASEMA: Juu ya walimu wa uongo, Yesu Kristo alitoa angalisho hili: ‘Kwa matunda yao mutawatambua. . . . Kila muti muzuri unazaa matunda mazuri, lakini kila muti uliooza unazaa matunda yasiyofaa.’ (Mathayo 7:15-18) Kati ya “matunda [hayo] yasiyofaa,” tunaweza kutaja kujiingiza katika siasa na kuitika matendo yenye kumuchukiza Mungu, kama vile mwanaume kulala na mwanaume ao mwanamuke kulala na mwanamuke. (Yohana 15:19; Waroma 1:25-27) Tena, kufundisha watu mafundisho na desturi zenye hazina maana kuliko kuwafundisha mafundisho ya muzuri yenye kuwa katika Maandiko ni kati ya matunda hayo yasiyofaa. (Mathayo 15:3, 9) Yesu alisema hivi: “Lisha kondoo wangu wadogo.” (Yohana 21:17) Lakini, leo watu wengi wako na njaa sana ya kiroho.

  • Dini na feza: Kulingana na Kituo cha Utafiti cha Pew, watu wengi wanaona kuwa dini inakazia sana feza. Shida kubwa zaidi ni kwamba, tofauti na waamini wao, viongozi fulani wa dini wanaishi maisha ya hali ya juu sana. Kwa mufano, katika muji mumoja wa Ujerumani kwenye watu wengi wanaoenda kwenye kanisa wako na shida ya kupata mambo ya lazima katika maisha, askofu ameshitakiwa kuwa anaishi maisha ya hali ya juu sana. Maisha hayo yamekwaza Wakatoliki wengi katika muji huo. Pia, ripoti moja ya gazeti GEO inasema kama katika inchi ya Nigeria, “kwenye watu milioni 100 wanaishi na feza dola moja hivi kwa siku, maisha ya hali ya juu sana ya mapasta fulani yanaanza kukwaza watu.”

    MAMBO BIBLIA INASEMA: Paulo,muandikaji mumoja wa Biblia aliandika hivi: “Sisi si wachuuzi wa [hatuuzishe] neno la Mungu.” (2 Wakorintho 2:17) Hata kama Paulo alikuwa mutumishi mwenye alijulikana katika kutaniko la Kikristo la wakati wa mitume, mara nyingi alifanya kazi ya mikono ili asiwekee wengine muzigo. (Matendo 20:​34) Kufanya hivyo kulionyesha kama alitii amri hii ya Yesu: ‘Mulipokea bure, mutoe bure.’—Mathayo 10:7, 8.

Mashahidi wa Yehova wanafuata kanuni hizo, hawauzishe vichapo vyao ao kulipisha mafundisho ya Biblia. Tena hawaombe sehemu ya kumi, wala hawakusanye ­sadaka kwenye mikutano yao. Lakini, feza zenye wako nazo lazima ili kuendesha kazi yao zinapatikana kupitia michango yenye watu wanatoa kwa kupenda.—Mathayo 6:2, 3.

Kuachana na Dini Kulitabiriwa Zamani!

Miaka fulani iliyopita, ingekuwa vigumu kuwazia hali mbaya yenye kupata dini leo. Lakini, Mungu aliona jambo hilo mbele ya wakati na alilionyesha katika Biblia. Kwa kutumia maneno ya mufano, Mungu alifananisha dini zote zenye kukosa uaminifu kwake na kahaba mwenye kujipodoa sana mwenye kuitwa ‘Babiloni Mukubwa.’—Ufunuo 17:1, 5.

Ufananisho huo ni wenye kufaa kwa sababu hata kama dini za uongo zinasema kuwa zinamutumikia Mungu kwa uaminifu, zimejiunga na watawala wa ulimwengu ili zipate nguvu na utajiri. Andiko la Ufunuo 18:9 linasema hivi: ‘Wafalme wa dunia walifanya uasherati pamoja naye.’ Tena, neno “Babiloni” linafaa, kwa sababu mafundisho na desturi za uongo za dini, kama vile kutokufa kwa nafsi, fundisho la utatu, na uchawi, yalianzia katika Babiloni ya zamani, muji wenye ulikuwa unajaa dini ya uongo na kuamini mambo ya uchawi. *Isaya 47:1, 8-11.

Muji wenye nguvu wa Babiloni ulianguka wakati maji yake ya ulinzi ‘yalikaushwa.’ Maji hayo ni mufereji wenye ulikuwa unapata maji kutoka kwenye Muto Efrati, na kukaushwa kwa maji hayo kulisaidia majeshi ya Wamedi na Waajemi kupata ushindi juu ya muji huo. (Yeremia 50:1, 2, 38) Kwa kweli, muji wa Babiloni ulikamatwa katika usiku mumoja!—Danieli 5:7, 28, 30.

Babiloni Mukubwa naye ‘anakaa juu ya maji mengi.’ Biblia inatuambia kama maji hayo yanamaanisha “vikundi vya watu na umati,” ni kusema, mamilioni ya watu ­wenye kuunga mukono dini za uongo. (Ufunuo 17:1, 15) Biblia ilitabiri kama maji hayo ya mufano yatakauka, jambo hilo linaonyesha uharibifu wa haraka na wenye kuwa karibu wa Babiloni wa leo. (Ufunuo 16:12; 18:8) Lakini ni nani atamuharibisha? Viongozi wa kisiasa wenye anajiunga nao, ambao upendo wao kwake utageuka kuwa chuki. Pia, watakamata mali yake yote, ao kula nyama yake ya mufano.—Ufunuo 17:16, 17. *

Maji yenye kupunguka yaliyozunguka Babiloni yanafananisha kutoka kwa watu katika Babiloni Mukubwa

‘Mutoke Kwake’!

Kwa sababu ya mambo yenye yatapata Babiloni Mukubwa, kwa upendo, Mungu anatoa angalisho hili: ‘Mutoke kwake, watu wangu, ikiwa hamutaki kushiriki pamoja naye zambi zake, na ikiwa hamutaki kupokea sehemu ya mapigo yake.’ (Ufunuo 18:4) Ona neno “ikiwa,” lenye kutajwa mara mbili katika andiko hilo. Kwa kweli, Mungu anatoa angalisho hilo kwa watu wenye wanahangaishwa na mafundisho yenye kutenganisha watu na Mungu na wenye wanataka kukubaliwa na yeye, watu kama vile Gaffar na Hediye, wenye tumekwisha kutaja.

Mbele Gaffar ajifunze Biblia, alimuona Mungu kuwa mutu mwenye tunapaswa kutii kwa sababu tu ya woga. Alisema hivi: “Nilitulizwa sana kujua kama Yehova ni Mungu wa upendo, na kama anataka tumutii kwanza kwa sababu ya upendo.” (1 Yohana 4:8; 5:3) Hediye alipata amani ya moyoni wakati alijua kama haiko Mungu ndiye alimufanya yatima, na kama hali yake haikupangwa mbele ya wakati. Alitiwa moyo na maandiko ya Biblia kama vile andiko la Yakobo 1:13, lenye kusema kama Mungu hajaribu watu kupitia mambo mabaya. Yeye na Gaffar waliitika mafundisho ya Biblia na wakatoka katika “Babiloni.”—Yohana 17:17.

Wakati Babiloni Mukubwa ataharibiwa, watu wenye wameonyesha utii kwa kutoka kwake ili ‘kuabudu Baba kwa roho na kweli’ hawatapatwa na jambo lolote mbaya. (Yohana 4:23) Watu hao wako na tumaini la kuona dunia ‘inajaa na kumujua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.’—Isaya 11:9.

Ndiyo, dini ya uongo na matunda yake mabaya vitaisha, kwa sababu Mungu ‘hawezi kusema uongo.’ (Tito 1:2) Lakini ibada ya kweli itaendelea milele!

^ fu. 16 Ili kupata habari zingine juu ya Babiloni Mukubwa, mambo Biblia inasema juu ya hali ya wafu, namna Mungu iko, na uchawi, soma kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? Unaweza kupata kitabu hicho kwenye adresi yetu ya Internete www.dan124.com/swc.

^ fu. 18 Soma habari “Mawazo ya Biblia—Mwisho wa Dunia,” katika gazeti hili la Amuka!