Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kwa Nini Ujifunze Kutoka kwa Mungu?

Kwa Nini Ujifunze Kutoka kwa Mungu?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Kwa Nini Ujifunze Kutoka kwa Mungu?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Kwa nini ujifunze kutoka kwa Mungu?

Mungu ana habari njema za jambo bora kwa ajili ya wanadamu. Anatueleza kuzihusu katika Biblia. Biblia ni kama barua ambayo tumeandikiwa na Baba yetu wa mbinguni.—Soma Yeremia 29:11.

2. Habari njema ni nini?

Wanadamu wanahitaji serikali nzuri. Hakuna mtawala wa kibinadamu ambaye amewahi kumwondolea mwanadamu jeuri, ukosefu wa haki, magonjwa, au kifo. Lakini kuna habari njema. Mungu atawapa wanadamu serikali nzuri ambayo itawaondolea mambo yote yanayofanya wateseke.—Soma Danieli 2:44.

3. Kwa nini ni muhimu kujifunza kutoka kwa Mungu?

Karibuni Mungu atawaondoa duniani watu wanaosababisha kuteseka. Sasa anawafundisha mamilioni ya watu wapole ili wafurahie maisha bora, yanayotegemea upendo. Watu wanajifunza katika Neno la Mungu jinsi ya kupambana na matatizo, jinsi ya kupata furaha ya kweli, na jinsi ya kumpendeza Mungu.—Soma Sefania 2:3.

4. Mtungaji wa Biblia ni nani?

Biblia ina vitabu vidogo 66. Viliandikwa na wanaume 40 hivi. Vitabu vitano vya kwanza viliandikwa na Musa, miaka 3,500 hivi iliyopita. Kitabu cha mwisho kiliandikwa na mtume Yohana, zaidi ya miaka 1,900 iliyopita. Lakini waandikaji wa Biblia waliandika mawazo ya Mungu bali si mawazo yao wenyewe. Kwa hiyo, Mungu ndiye Mtungaji wa Biblia.—Soma 2 Timotheo 3:16; 2 Petro 1:21.

Tunajua kuwa Biblia imetoka kwa Mungu kwa sababu inatabiri mambo ya wakati ujao kwa usahihi kabisa. Hakuna mwanadamu anayeweza kufanya hivyo. (Isaya 46:9, 10) Pia, Biblia inatufunulia sifa za Mungu. Ina nguvu za kubadili maisha ya watu kuwa bora. Mambo hayo yanawathibitishia mamilioni ya watu kuwa Biblia ni Neno la Mungu.—Soma Yoshua 23:14; 1 Wathesalonike 2:13.

5. Unaweza kuielewa Biblia jinsi gani?

Yesu alikuwa mwalimu mashuhuri wa Neno la Mungu. Ingawa watu wengi aliozungumza nao waliijua Biblia, walihitaji kusaidiwa ili kuielewa. Ili kuwasaidia, Yesu alitaja andiko moja la Biblia baada ya lingine na kueleza “maana ya Maandiko” hayo. Makala hii, “Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu,” itatumia njia hiyohiyo kukusaidia.—Soma Luka 24:27, 45.

Ni mambo machache yanayosisimua zaidi kuliko kujifunza kutoka kwa Mungu kuhusu kusudi la uhai. Lakini huenda watu fulani wasifurahi kuona kuwa unasoma Biblia. Usivunjike moyo. Tumaini lako la kufurahia uzima wa milele linategemea kumjua Mungu.—Soma Mathayo 5:10-12; Yohana 17:3.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 2 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.